BARAZA la Mitihani la Tanzania (NECTA), limetangaza matokeo ya mtihani wa kidato cha nne uliofanyika Novemba 2023, ambapo watahiniwa 484,823 (87.65%) wamefaulu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Akitangaza matokeo hayo, leo tarehe 25 Januari 2024, Katibu Mtendaji wa NECTA, Dk. Said Ally Mohamed, amesema watahiniwa wa kike wamefaulu wengi zaidi wakati wakiume wakifaulu vizuri.
“Ufaulu kwa ujumla umepanda ukiangalia asilimia zaidi ya 87 ya waliofaulu wametoka kwenye shule za Serikali, asilimia 13 kutoka shule binafsi,” amesema Dk. Mohamed.
Amesema katika mtihani wa 2023, kumekuwa na ongezeko la shule zilizopata wastani wa daraja la A mpaka D na A mpaka C ikilinganishwa na 2022. Ufaulu asomo ya sayansi ya jamii (Historia, Jiographia na Uraia), umeongezeka huku Kiswahili kikiongoza kwa kuwa na ufaulu wa asilimia 96.8 katika alama A.
Somo la hisabati nalo ufaulu wake umeongezeka kwa asilimia 5.4 kutoka asilimia 20.08 mwaka 2022 hadi kufikia asilimia 25.08 mwaka 2023.
Katika hatua nyingine, Dk. Mohamed amesema watahiniwa 102 wamefutiwa matokeo kwa makosa ya udanganyifu na kuandika matusi, huku 376 matokeo yao yakizuiliwa baada ya kupata matatizo ya kiafya na kushindwa kufanya mitihani.
“Wapo watahiniwa wamesaidiana humo ndani wamekamatwa, lakini ipo kesi moja mwalimu mkuu amesaidia watahiniwa wake hilo litafanyiwa kazi kwa kuchukuliwa hatua za kinidhamu,” amesema Dk. Mohamed.
Leave a comment