Mbunge wa Buchosa, Eric Shigongo (CCM), ameitaka Serikali kutoa elimu kwa jamii kuhusu udhibiti wa mamba pamoja na kuendelea kujenga uzio katika sehemu za kuchota maji ili kuzuia vifo vinavyosababishwa na wanyama hao. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Shigongo ametoa kauli hiyo leo Ijumaa bungeni jijini Dodoma katika swali alilouliza kuhusu mpango wa serikali kuhusu ujenzi wa uzio huo.
Akijibu swali hilo na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii amesema wizara inajenga uzio (vizimba) vya mfano kwa ajili ya kuzuia mamba katika maeneo mbalimbali nchini ambayo yana changamoto ya mamba.
Amesema kwa upande wa Jimbo la Buchosa, Wizara imejenga vizimba viwili vyenye thamani ya Sh 60,470,000 katika vijiji vya Kanyala na Izindabo vilivyopo Kata za Bulyaheke na Lugata kwenye Tarafa ya Buchosa.
“Halmashauri za wilaya zinahimizwa kujenga vizimba katika maeneo yenye changamoto ya Mamba. Wizara inatoa rai kwa Waheshimiwa Wabunge kuzihimiza Halmashauri zao kutenga bajeti itakayowezesha ujenzi wa vizimba katika maeneo yao pia wizara itatoa wataalam kwa ajili ya kusimamia ujenzi wa vizimba hivyo,” amesema.
Aidha akiuliza swali la nyongeza Mbunge wa Magu, Boniventura Kiswaga alitaka kufahamu mpango wa kuwapunguza mamba hao pamoja na mkakati wa kutoa elimu ili wasiwasumbue wananchi.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri huyo, amesema kuna mikakati ya aina mbili ambayo kwanza ni uvunaji wa kitalii pamoja na kutoa elimu jinsi ya kutumia maeneo ya maziwa na mito yenye mamba wengi.
“Tunawapa elimu na kuwasisitiza kuacha kufuata huduma za maji usiku kwenye maziwa na mito yenye mamba ili kuwakwepa wanyama hao,” amesema.
Leave a comment