SERIKALI imeombwa kuzipunguzia mzigo wa kodi shule binafsi ili zimudu gharama za uendeshaji kwa lengo la kutoa huduma bora za elimu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Ombi hilo limetolewa leo tarehe 26 Agosti 2023, jijini Dar es Salaam na Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya shule hiyo, Salva Rweyemamu, akizungumza katika mahafali ya 25 ya wanafunzi wa darasa la saba.
“Jambo moja nadhani Serikali lazima ijipange, watupunguzie kodi. Unajua sekta binafsi lazima ishamiri… unavyoanza kuipiga kodi unaiua kwa sababu biashara hii ni tofauti na hizo zinazoweza kulipa kodi kama kuuza matofali na kadhalika. Elimu ni kama afya na ifike mahali taasisi lazima ziweze kukua na ili zikue inabidi uzipunguzie kodi kwanza sababu wengine wamekopa kuzianzisha,” amesema Rweyemamu.
Katika hatua nyingine, Rweyemamu amesema shule hiyo inaendelea kuiunga mkono Serikali katika masuala mbalimbali, ikiwemo kutoa wahitimu waliofundishwa uzalendo wa kuijenga nchi.
Aidha, Rweyemamu amewataka wazazi na walezi kuendelea kuiunga mkono shule hiyo, ili iendelee kudumu.

“Tunawashukuru wazazi waliotukabidhi watoto hawa tangu awali hadi sasa wanahitimu na naomba muendelee kutuunga mkono na kutuamini sababu tuna miaka 25, ni miaka mingi kama taasisi hivyo muendelee kuiunga mkono shule mpaka miaka ijayo,” amesema Rweyemamu.
Awali, Mkuu wa Shule ya Msingi Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Maria Massai, amesema shule hiyo inaendelea kuenzi misingi ya baba wa taifa, ikiwemo kuwafundisha wanafunzi kujiepusha na vitendo vya ubaguzi na kuwa wazalendo.
Wakisoma risala kwa wageni waalikwa, baadhi ya wanafunzi wanaotarajia kuhitimu darasa la saba, walisema katika kipindi cha miaka saba walichosoma shuleni hapo, wamefanikiwa kujifunza mambo mbalimbali, ikiwemo namna ya kutumia rasilimali endelevu, kkilimo na utunzaji wa mazingira.
Leave a comment