RAIS Samia Suluhu Hassan leo jumapili amewaonya viongozi wa umma kuacha ‘kujidogosha’ kwa kutekeleza majukumu yao kwa kusubiri maelekezo kutoka juu badala yake wawe wabunifu na kufanya kazi kwa kuzingatia kanuni, miongozo, sheria na mipango ya Serikali. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea.)
Kauli hiyo ya Rais imekuja baada ya viongozi wengi wa umma kuogopa kufanya maamuzi sahihi kwa wakati sahihi katika utekelezaji wa majukumu yao na kubaki kusubiri maagizo kutoka juu.
Rais Samia maagizo hayo leo tarehe 27 Agosti 2023 wakati akifunga mafunzo kwa Wakuu wa Mikoa na Makatibu Tawala wa Mikoa, yaliyofanyika katika Taasisi ya Uongozi ya Mwalimu Nyerere, Kibaha mkoani Pwani.
Amesema katika uongozi wake hatashusha maelekezo kwa viongozi hao kuhusu nini wanapaswa kufanya, badala yake anataka kuwaona wanakuwa na ndoto kulingana na mipango ya Serikali.
Amewataka viongozi hao wasisubiri Rais aseme Mkuu wa Mkoa fanya hili huko kwani hiyo ilikuwa dhana iliyojengeka zamani.
“Enzi za Mwanri (Mkuu wa Mkoa wa zamani wa Tabora) mimi napenda kuona mtu anajituma, anajielewa anajua nini anafanya,” amesema na kuongeza;
“Kwenye ndoto zako hizo usiyumbishwe unatakiwa kuwa na hoja za kujitetea iwapo unachokifanya kitahojiwa,” amesema.
Aidha, amewataka viongozi hao kusimamia maamuzi yao, huku akionya hilo lisiwafanye kutokubali ushauri wa wengine.
“Naposema kusimama kwenye maamuzi yako sio muende huko kichwa ngumu mnachotaka ndo hicho hicho, hapana, unaangalia mazingira yaliyopo na unafanya kulingana na miongozo ya kisheria,” amesema.
Leave a comment