RAIS Samia Suluhu Hassan leo jumapili amemtumbua Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, Hanafi Msabaha kutokana na madai ya kusababisha baadhi ya wananchi wa eneo hilo kurejesha kadi za Chama Cha Mapinduzi (CCM) baada ya kuwabagua katika miradi inayotekelezwa na Serikali. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).

Rais Samia amesema Mkuu huyo wa wilaya alijitetea kuwa wananchi hao wapo kwenye eneo la ngome ya upinzani ilihali akifahamu ya kuwa hata kama ni wafuasi wa chama cha upinzani wote ni Watanzania na wanahitaji kupelekewa miradi inayotekelezwa na Serikali yao.
Rais Samia ametangaza kuchukua uamuzi huo leo Jumapil wakati akifunga mafunzo kwa Wakuu wa Mikoa na Makatibu Tawala wa Mikoa, yaliyofanyika katika Taasisi ya Uongozi ya Mwalimu Nyerere, Kibaha mkoani Pwani.
Amesema kamwe hawezi kumvumilia mkuu wa wilaya au mkoa anayehamisha miradi ya serikali kutoka kwa wananchi wenye uhitaji mkubwa na kupeleka kwa wananchi wenye uhitaji mdogo bila sababu za msingi.
“Mkuu wa Wilaya anahongwa, mradi anaacha kwenda unakotakiwa anapeleka usipotakiwa, kiasi kwamba wananchi wanafika kurudisha kadi za chama, sisi huku tuna haja kubwa mmetuacha fedha mmepeleka kule na kadi zenu hizo.
“Sina imani na Mkuu wa Wilaya anayesababisha kadi zirudishwe, Mtwara, Mkuu wa Wilaya yako sijui Hanafi (Msabaha) namtimua leo siwezi kustahimili kadi za chama zinarudishwa, nini Mkuu wa Wilaya yupo DED yupo yeye na DED wake,” amesema.
“Watu wana shida anaulizwa anasema unajua kule wengi wapinzani, so what si Watanzania wale? Kwani wao sio watu, tena wamejenga maana kigezo ilikuwa wajenge atakayefika mbali ndiyo mradi upelekwe kwake,” ameeleza.
Bila kutaja aina ya mradi ambao umehamishwa huko wilayani Mtwara, Rais Samia amesema baadhi ya wakuu wa mikoa wanawabeba wakuu wa wilaya ambao hawakai kwenye vituo vyao vya kazi.
Amesema baadhi ya wakuu wa wilaya wanasafiri kila siku kwenda kwenye maeneo wanakosaka ubunge ilihali mkuu wa mkoa anaona bila kuchukua hata hatua ya kumuandikia Waziri au Rais barua kumshtakia mkuu huyo wa wilaya.
Ameongeza kuwa mashtaka mengi ni ya watendaji wa ngazi za chini huku watendaji wa ngazi za juu kama wakuu wa wilaya wakiachwa kuendelea kutumia vyeo vyao kujinufaisha.
Leave a comment