RAIS Samia Suluhu Hassan amefanya uteuzi, utenguzi na uhamisho wa viongozi mbalimbali ikiwamo mbalimbali. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Katika taarifa iliyotolewa leo tarehe 18 Desemba 2023 na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Zuhura Yunus imesema amemteua Balozi Meja Jenerali Paul Kisesa Simuli kuwa Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Uganda.
Amemteua Selwa Abdalla Hamid kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Igunga. Hamid anachukua nafasi ya Athman Francis Msabila ambaye amesimamishwa kazi. Kabla ya uteuzi huu, Hamid alikuwa Meneja Miradi, Bohari Kuu ya Dawa (MSD).
Amemteua Mariam K. H. Chaurembo kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mji wa Tunduma. Chaurembo anachukua nafasi ya Lena Martin Nkya ambaye uteuzi wake umetenguliwa.
Kabla ya uteuzi huu, Chaurembo alikuwa Afisa Utumishi Mkuu, Wizara ya Nishati na amewahi kuwa Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyang’wale.
Amemteua Fabian Manoza Said kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya ya Momba. Said anachukua nafasi ya Butamo Nuru Ndalahwa ambaye uteuzi wake umetenguliwa.
Kabla ya uteuzi huu, Said alikuwa Afisa Usimamizi Mkuu wa Mitihani, Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Mkwawa na amewahi kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Meatu.
Amemteua Dk. Khamis Hassan Mwinyimvua kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Usafiri wa Anga, Tanzania. Dk. Mwinyimvua ni Mhadhiri Mwandamizi, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na anachukua nafasi ya Prof. Longinus K. Rutasitara ambaye amemaliza muda wake.
Uhamisho
Amemhamisha kituo cha kazi Dk. Peter Maiga Nyanja, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Muleba kwenda kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Wanging’ombe.
Nyanja anachukua nafasi ya Maryam Ahmed Muhaji ambaye hivi karibuni aliteuliwa kuwa Katibu Tawala wa Manyara. Uteuzi na uhamisho huu unaanza tarehe 18 Desemba 2023.
Leave a comment