Rais Samia Suluhu Hassan amekabidhi tuzo ya heshima kwa benki ya Taifa ya Biashara (NBC) ikiwa ni ishara ya kutambua mchango wa benki hiyo katika kufanikisha msimu wa 17 wa tuzo za Rais za Wazalishaji Bora wa Viwanda (PMAYA).
Pia NBC Iimepata tuzo hiyo kwa kuchochea kasi ya ukuaji wa sekta ya viwanda nchini kwa ujumla kupitia huduma zake za kifedha. Benki ya NBC ni mdhamini mkuu wa tuzo hizo za kila mwaka kwa mwaka wa pili mfululizo. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Rais Samia alikabidhi tuzo hiyo kwa Mkurugenzi Mtendaji wa benki ya NBC, Theobald Sabi wakati wa hafla ya utoaji wa tuzo hizo iliyofanyika jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki.
Tuzo za PMAYA huandaliwa na Shirikisho la Wenye Viwanda Tanzania (CTI) zikilenga kutambua mchango wa sekta ya viwanda kiuchumi na kuchochea ushindani wa utoaji huduma miongoni mwa viwanda hivyo.
Akizungumza kwenye hafla hiyo, Rais Samia pamoja nakuwapongeza wadhamini mbalimbali wa tuzo hizo ikiwemo benki ya NBC, aliangazia masuala mbalimbali yanayohusu mustakabali wa sekta viwanda nchini hususani suala la upatikanaji wa nishati ya umeme wa uhakika huku pia akionyesha kutambua mchango na umuhimu wa huduma za kifedha katika kukuza ustawi wa sekta ya viwanda na kuchochea ushindani katika soko la ndani na nje ya nchini.
“Najua kuna changamoto ya upatikanaji wa dola lakini nashukuru kuona kwamba kupitia jitihada mbalimbali zinazoendelea kufanywa na wataalamu wetu wa masuala ya fedha ndio zimetusaidia kukabiliana na changamoto ya upatikanaji wa dola. Kwasasa tunaweza kutoa hadi dola milioni 2 kwa mtu mmoja kwa siku kutoka kiwango cha utoaji wa dola laki 5 kwa mtu mmoja kwa siku katika kipindi ambacho hali ilikuwa mbaya zaidi,” alisema Rais Samia.
Pia alibainisha kuwa hatua hiyo ni kubwa ikilinganishwa na baadhi ya mataifa jirani ambayo kwasasa yanashindwa kutoa hata dola laki 5 kwa mtu mmoja kwa siku.
Hata hivyo, alisema serikali inafanya jitihada mbalimbali kuhakikisha inaongeza upatikanaji wa dola nchini ikiwemo kuhamasisha ongezeko la bidhaa zinazouzwa nje ya nchi hususani kupitia mauzo ya bidhaa zinazozalishwa kupitia sekta za viwanda na kilimo hususani kilimo cha mboga mboga (horticulture).
Awali akizungumza kwenye hafla hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC, Theobald Sabi alisema benki hiyo imejipanga katika utoaji wa huduma na fursa mbalimbali kwa wadau wa sekta ya viwanda nchini.
Pia imejipanga kutoa mikopo ya aina zote hususani ile inayolenga kuongeza uzalishaji viwandani, huduma za bima nak inga dhidi ya majanga na mabadiliko ya riba, huduma za malipo ya ndani na nje ya nchi ikiwemo ukusanyajaji wa mapato ya serikali pamoja na utoaji wa mikopo inayowezesha biashara za kimataifa (International Trade Financing).
“Pamoja na huduma kibenki kwa wadau wa viwanda, NBC kwasasa tunatekeleza mkakati wetu wa kukuza huduma rasmi za kibenki kwa makundi maalumu ikiwemo wafanyabiashara wadodo na wa kati (SMEs), wanawake pamoja na wajasiriamali,’’ alibainisha Sabi
Kwa mujibu wa Sabi ushirikiano baina ya wadau wakubwa wa viwanda na makundi hayo maalum utachochea zaidi kasi ya ukuaji wa Uchumi nchini kutokana na muingiliano mkubwa baina yao.
Aidha, Sabi ambae pia ni Mwenyekiti wa Umoja wa Mabenki Tanzania (TBA) alitumia fursa hiyo kuwasilisha kwa Rais Samia utayari wa taasisi zote wananchama wa umoja huo katika kuhudumia sekta ya viwanda nchini.
Pia alipongeza jitihada mbalimbali zinazofanywa na serikali katika kuweka mazingira rafiki ya biashara ili kufungua nchi kiuchumi na kuvutia uwekezaji.
“Jitihada hizi za serikali zinazoonekana katika maeneo mengi ikiwemo utalii, miundombinu, mauzo ya bidhaa za nje (Export), ukuaji wa sekta madini na maeneo mengine mengi ni matunda ya juhudi hizo za serikali ambazo zimezaa fursa kubwa kwa taasisi za fedha nchini…tunashukuru sana Mheshimiwa Rais,’’ alipongeza Sabi.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa CTI, Paul Makanza alionyesha kuguswa zaidi na ushirikiano uliopo baina ya wadau wa viwanda nchini pamoja na serikali kama ilivyo pia baina ya wadau hao na taasisi za fedha nchini.
Pamoja na mambo mengine aliipongeza benki ya NBC kwa namna inavyoshirikiana na wadau hao kupitia huduma zake pamoja na udhamini wa benki hiyo kwenye matukio mbalimbali yanayoandaliwa na wadau hao ikiwemo Maonesho ya Kimataifa ya Viwanda (TIMEXPO) na tuzo za PMAYA.
Leave a comment