WABUNGE Viti Maalum 19, waliovuliwa uanachama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), bado hawajafanya maamuzi juu ya hukumu iliyotolewa na mahakama dhidi ya kesi waliyofungua kupinga kufukuzwa na chama hicho. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Hayo yamebainishwa leo tarehe 19 Disemba 2023 na Wakili wa wabunge hao, Edson Kilatu, alipoulizwa na MwanaHALISI Online uamuzi wa wateja wake baada ya Mahakama Kuu, Masjala Kuu ya Dar es Salaam, kutoa hukumu hiyo mbele ya Jaji Cyprian Mkeha.
Hukumu hiyo iliyotolewa Alhamisi iliyopita, ulibariki uamuzi wa Kamati Kuu ya Chadema kuwafukuza wabunge hao, huku ikibatilisha uamuzi wa Baraza Kuu la chama hicho kutupilia mbali rufaa zao walizokata kupinga kutimuliwa Chadema.
Akizungumza na mtandao huu, Wakili Kilatu amesema bado hawajamaliza mazungumzo na wabunge hao wanaoongozwa na Halima Mdee, kujua kama wana nia ya kukata rufa kupinga hukumu hiyo, kwa kuwa baadhi yao wako nje ya nchi.
“Bado tunazungumza, unajua wateja wetu wengine wako Burundi kwenye michezo ya Bunge hawajarudi. Tunataka wakirudi ambapo tunategemea watarudi ndani ya siku mbili tatu tutakaa kikao kwa pamoja tushauriane tuone kama tutachukua hatua zaidi au wakiridhika tutaacha maana ndiyo wenye kibali cha kukata rufaa. Tunaamini mpaka mwisho wa wiki hii tutakuwa tumepata majibu,” amesema Wakili Kilatu.
Alipoulizwa kama wateja wake wataendelea kuwepo bungeni jijini Dodoma kufuatia uamuzi huo, Wakili Kilatu alijibu akisema bado wataendelea kuwepo hadi pale baraza kuu la Chadema litakapotekeleza amri ya mahakama ya kurudia kusikiliza na kutoa uamuzi dhidi ya rufaa zao.
Wakili Kilatu amesema, kina Mdee wataendelea kubaki bungeni kwa mujibu wa kifungu cha 6C (5) cha Sheria ya Vyama vya Siasa, ambacho kinasema hakuna mwanachama atakaehesabika ametukuzwa hadi michakato yote inayotambuliwa na katiba ya chama chake itakapokamilika.
“Maana yake michakato ili ikamalike inabidi mpaka rufaa ikamilike ndipo unasema mchakato wa kuwavua uanachama umekamilika. Sasa kwa sababu maamuzi ya baraza kuu tayari yamefutwa na mahakama maana yake haijaisha na chama kimeagizwa kiwasikilize upya,” amesema Wakili Kilatu.
Wakili Kilatu amedai “uwepo wao kwenye Bunge hauna mjadala ni wa halali kwa mujibu wa sheria na katiba ya chama chao. Ukisema mfano leo uwaondoe bado chama hakijasikiliza rufaa yao ina maana mbili, moja umetoa maamuzi ya kuwahukumu wakati baraza halijakaa wa kuwafukuza lakini pili unatengeneza mazingira ya kumhukumu bila kumsikiliza na kwamba endapo atakuwa hana hatia hutaweza kumfidia kwa athari ulizompa.”
Leave a comment