RAIS Samia leo tarehe 14 Machi 2022 ameteua viongozi mbalimbali wa Serikali huku akimwondoa Humphrey Polepole bungeni na kumpeleka kuwa balozi wa Tanzania nchini Malawi.
Pia amemrejesha Nehemiah Mchechu kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) ikiwa ni miaka mitatu imepita tangu kutenguliwa katika nafasi hiyo na Hayati Rais John Magufuli. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Zuhura Yunus, Rais Samia amemteua Shamsi Vuai Nahodha kuwa mbunge wa bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Taarifa hiyo imeeleza pia Rais amemteua aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), Waziri Kindamba Waziri kuwa Mkuu wa Mkoa wa Njombe akichukua nafasi ya Mhandisi Marwa Mwita Rubya ambaye amestaafu kwa umri.
Aidha amewateua balozi na Mkuu wa Jeshi la Polisi mstaafu Ernest Mangu kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) na Meja Jenerali John Mbungo kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Kampuni ya Meli Tanzania (MSCL).
Vile vile amemteua Peter Rudolph Ulanga kuwa Mkurugenzi Mkuu wa TTCL. Kabla ya uteuzi huo Ulanga alikuwa Mkurugenzi Mstaafu wa Mfuko wa Mawasiliano kwa wote (UCSF).
Taarifa hiyo imeeleza kuwa Polepole na Kindamba wataapishwa kesho saa nne asubuhi katika viwanja vya Ikulu Chamwino Dodoma.
Leave a comment