WIZARA ya Maji, imeagizwa kukamilisha zoezi la kubadilisha mita za maji kutoka zile zinazotumika sasa za malipo baada ya matumizi na kuziweka mpya za malipo kabla ya matumizi, ili kudhibiti changamoto ya wananchi kubambikiwa bili. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Agizo hilo limetolewa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, leo Alhamisi, Ikulu jijini Dar es Salaam, akimuapisha Naibu Waziri wa Maji, Kundo Mathew, pamoja na viongozi wengine aliowateua hivi karibuni.
Katika hatua nyingine, Rais Samia ameagiza wizara hiyo ikakamilishe miradi ya maji ili kutekeleza maelekezo ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), ya huduma hiyo kupatikana kwa asilimia 95 maeneo ya mijini na asilimia 85 vijijini ifikapo 2025.
“Bili za maji ni kilio kingine cha wananchi, tumelia sana kubambika bili za maji naomba fanyeni kama wanavyofanya TANESCO mwekeeni mtu mita yake ya maji atumie alichokilipa pesa yake ikimalizika mita inakata atakwenda kuyanunua mengine apate kutumia,” amesema Rais Samia na kuongeza:
“Lakini unamuachia katumia unakuja kutizama hapa katumia 40 unamuandikia 80 na bili yako ya nyumbani umemtilia yeye, hapana taufuteni mita ambayo watalipa jinsi watakavyotumia, hilo ndilo agizo langu na nasikia mmeshawahi kuziagiza zimepimwa nendeni kafungeni hizo mita wananchi wapate imani walipe kile wanachokitumia.”
Leave a comment