MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Arusha nchini Tanzania, kesho Ijumaa tarehe 1 Oktoba 2021, itatoa hukumu ya kesi ya unyang’anyi wa kutumia silaha, Na. 105/2021, inayomkabili aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya na wenzake wawili. Anaripoti Mwanaharusi Abdallah, TUDARCo … (endelea).
Tarehe hiyo ilipangwa Jumanne ya tarehe 24 Agosti 2021 na Hakimu Mkazi Mwandamizi, Odira Amworo, baada ya mahakama hiyo kumaliza kusikiliza ushahidi wa pande zote mbili.
Mbali na Sabaya, washtakiwa wengine ni, Sylvester Nyegu na Daniel Mbura, ambao wanadaiwa kuvamia na kufanya unyang’anyi wa kutumia silaha wa zaidi ya Sh. 2.7 milioni, katika duka la Mohamed Saad, tarehe 9 Februari 2021.
Shahidi wa mwisho upande wa utetezi, ambaye alitoa ushahidi wake, alikuwa ni Mbura, akiongozwa na jopo la mawakili wa utetezi, likiongozwa na Wakili Dancan Oola.
Baada ya ushahidi huo kufungwa, Wakili wa Serikali Mkuu, Tumaini Kweka, aliiomba mahakama hiyo itoe siku saba kwa pande zote mbili, kuwasilisha majumuisho ya kesi hiyo kwa njia ya maandishi.
Hakimu Amworo alikubali ombi hilo na kutoa siku saba kwa pande zote mbili, kuwasilisha majumuisho hayo.
Kesi hiyo, ilisikilizwa mfululizo kuanzia tarehe 19 Julai hadi 24 Agosti 2021. Ni baada ya Sabaya na wenzake, kusomewa maelezo ya awali ya kesi hiyo mhakamani hapo, tarehe 16 Julai 2021.
Sabaya alifikishwa mahakamani baada ya Rais Samia Suluhu Hassan kutangaza kumsimamisha tarehe 13 Mei 2021 ili kupisha uchunguzi wa tuhuma mbalimbali zilizokuwa zinamkabili.
Sabaya aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), Mkoa wa Arusha, anza safari ya kuwa mkuu wa wilaya ya Hai, tarehe 28 Julai 2018 na aliyekuwa Rais wa Tanzania, Hayati John Pombe Magufuli.
Lazima muheshim sheria na katiba ya nchi sio kujifanyia mambo ya kihuni kwa kisingizio (ulitumwa) nenda jela ili iwe fundisho kwa wengine watao jaribu kukubali maagizo yaliyo njee ya misingi ya katiba na sheria za nchi ambazo ulikula kiapo kuzilinda.