RAIS wa Kenya, William Ruto ametoa onyo kwa walanguzi wa biashara ya sukari nchini humo ambao wanazuia mchakato wa kutaka kufufuliwa kwa kampuni ya sukari ya Mumias akiwaeleza kuwa aidha, wahame au wasafiri kwenda mbinguni kwani atapambana nao bila kuchoka. Anaripoti Maryam Mudhihir…(endelea).
Ametoa onyo hilo wakati akizungumza na wananchi wa Kaunti ya Bungoma akiwa anatoa msimamo wake kuhusu kuendelezwa kwa kampuni hiyo ambayo inalegalega huku walanguzi wa sukari wakihusishwa kudumaza juhudi za Serikali kutaka kuifufua kampuni hiyo.

“Tayari tumewaambia watu hawa wote waondoke! Kampuni hii ni ya watu, na tunapanga kuifufua kwani hatumburudishi mtu yeyote. Tayari nimewapa chaguzi tatu; ama wanaondoka nchini, nitawafunga, au wasafiri na kwenda mbinguni,” alisema Rais.
Katika hatua nyingine Seneta wa Kaunti ya Kisii, Richard Onyonka amepinga kauli za Rais Ruto akimtaka kuwapa nafasi watuhumiwa ya kujieleza au kuwafikisha katika Mahakama ya Sheria kwa hatua stahiki.
“Ningependa kumsihi Rais wetu, matendo yake na matamshi yake yana maana ya kitu kibaya kinachoweza kuwatokea.
“Rais anaposimama na kuzungumza kuhusu mtu binafsi, mtu huyo, iwe amevunja sheria au la, amewekwa katika nafasi ambayo naona ukosefu wa haki,” alisema Onyonka.
Pia amemshauri Rais kutokuwa mtu wa kutoa vitisho hadharani kwani atakuwa anakwenda kinyume cha sheria za nchi huku akitaka mchakato huo ufanyike haraka ili haki ipatikane.
“Tunapaswa kuanza mchakato wa haraka sana. Kama kuna mtu amevunja sheria, basi apitie mchakato huo. Rais asiwe mtu anayetoa vitisho hadharani na kumtuhumu mtu binafsi,” aliongeza.
Kabla ya onyo hili la umma kwa walanguzi, alikuwa akiwatuhumu wafanyabiashara wa sukari akiwemo bilionea Singh Rai na wengine wenye nguvu waliozuia mipango yake ya kufufua tasnia ya sukari nchini Kenya.
Leave a comment