MKUU wa Mkoa Kusini Pemba, Amour Hamad Salehe, amekanusha taarifa zilizosambazwa kwenye mitandao ya kijamii kwamba Rais Samia Suluhu Hassan, ametoa sadaka ya Sh 5,000 kwa baadhi ya wakazi wa mkoa huo. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Katika taarifa aliyoitoa kwa vyombo vya habari jana Ijumaa amesema taarifa hizo ni uzushi na upotoshaji kwa sababu zoezi hilo halihusiani na Rais Samia kama inavyoelezwa kwenye mitandao ya kijamii.
“Kuna mfanyabiashara mmoja amekuwa na utamaduni zaidi ya miaka sita wa kutoa sadaka kwa watoto mayatima kila ifikapo mwezi mtukufu wa Ramadhani.
“Kwa awamu ya kwanza zoezi la utoaji sadaka lilifanyika kwa ufanisi mkubwa. Awamu ya pili wananchi walipeana taarifa iliyohamasisha wananchi kufika kwa wingi,” amesema.
Amesema waliokuwapo kwenye mpango huo walipata sadaka kama ilivyopangwa.
“Kwa ubinadamu wake wote waliokuwa nje ya mpango walipewa kila mmoja Sh 5,000 kama nauli ya kurejea nyumbani na sio sadaka,” amesema RC Amour.
Aidha, amesema mfanyabiashara huyo anayejulikana kwa jina la Abas Haji ambaye ni anayemiliki wa hoteli kwenye eneo la Mgogoni Pemba alimueleza kuwa; “msaada huu sio kutoka kwa Mama Samia wala Ikulu au watu wengine. Msaada huu ni mimi kama mimi na familia yangu.”
Leave a comment