MKUU wa Mkoa wa Dodoma, Antony Mtaka, ametoa siku 65 kwa Meneja wa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (Ruwasa) kukabidhi mradi wa maji kwa wananchi wa kijiji cha Mtera kata ya Mtera wilayani Mpwapwa wenye thamani ya Sh1.7 bilioni. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…(endelea)
Mtaka ametoa agizo hilo jana Jumatatu tarahe 18 Julai, 2022 mara baada ya kufanya ziara ya kukagua ujenzi wa mradi huo ambao umefikia asilimia 75.
Mtaka amesema kuwa miradi ya Serikali inayotekelezwa kwa manufaa ya wananchi inatakiwa kukamilishwa haraka ili wananchi waweze kunufaika nayo.
Mtaka amelazimika kuweka ukomo wa muda mradi huo kukamilika kutokana na wananchi wa kijiji cha Mtera kupeleka malalamiko kwake wakidai kuchelewa kwa mradi huo wa maji ambao unatakiwa kuhudumia watu zaidi ya 7,000 wa kijiji hicho.
Wananchi wakichangia katika mkutano huo walimshutumu Mhandisi wa Ruwasa Wilaya ya Mpwapwa, Crispian Warioba na meneja wa Ruwasa Mkoa wa Dodoma Dk.Godfret Mbambaya kuwa wamekuwa kikwazo katika kukamilisha mradi huo muhimu jambo ambalo linasababisha usumbufu mkubwa.
Mchungaji wa kanisa la Calvary Assembless Of God Tanzania, Jackos Madelemu, amesema kuwa kijiji cha Mtera kinakabiliwa na changamoto ya maji kutokana na wataalamu kutokuwa karibu na wananchi.
Sambamba na hilo alisema kutokana na umbali wa kutoka Mtera kwenda makao makuu ya Wilaya ni vyema Serikali ikaona umuhimu wa kuifanya Mtera kuwa wilaya au kuwa sehemu ya wilaya ya Chamwino badala ya kuendelea kuwa wilaya ya Mpwapwa.
Kutokana na hali hiyo Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mtaka amewaaka watendaji wa Ruwasa kuhakikisha wanapotekeleza miradi yao wanawashirikisha wananchi kila hatua wanayoifikia.
Pia amewataka kutekeleza miradi kwa kuwashirikisha wananchi na kuagiza wataalamu wa Ruwasa pamoja na watendaji wa vijiji na kata kutembelea miradi ya maendeleo mara kwa mara.
Leave a comment