Rais wa Serikali ya Mpito Mali, Assimi Goita, amenusurika kifo baada ya watu wasiojulikana kujaribu kutaka kumchoma kisu tumboni. Inaripoti BBC … (endelea).
Goita alikumbwa na mkasa huo alipokuwa msikitini, katika Mjii Mkuu wa nchi hiyo, Bamako, akishiriki swala ya Eid al-Adha.
Kwa mujibu wa mtandao huo, watu wawili wanashikiliwa na vyombo vya dola kwa tuhuma za kuhusika na tukio hilo.
Waziri wa Dini nchini Mali, Mamadou Kone, amesema watuhumiwa hao walijaribu kutaka kumuuwa rais huyo wa mpito, lakini hawakufanikiwa.
Amesema walioathirik ana tukio hilo ni watu wengine waliokuwepo katika swala hiyo.
Tukio hilo limetokea takribani miezi 11, tangu Goita aliyekuwa kiongozi wa jeshi nchini humo, kuipindua Serikali iliyokuwa madarakani chini ya Rais Ibrahim Keita.
Baada ya mapinduzi hayo, Goita alikabidhiwa umakamu wa rais katika Serikali mpito, iliyopewa muda wa miezi 18, kuanzia Oktoba 2020 hadi Aprili 2022. Iliyokuwa inaongozwa na Rais Bah Ndaw.
Goita alimuondoa madarakani kwa nguvu Ndaw, tarehe 24 Mei mwaka huu, akimtuhumu kwamba anataka kuhujumu makubaliano ya kuendesha Serikali ya mpito.
Ndaw alidaiwa kutotekeleza makubaliano ya kuandaa uchaguzi wa 2022, uliopangwa kwa ajili ya uchaguzi viongozi wa Serikali ya kiraia.
Pia, Goita alimtuhumu Ndaw kwamba, alipokuwa madarakani hamkushirikisha katika mabadiliko ya baraza la mawaziri.
Baada ya kumpindua Ndaw, Goita alitangazwa kuwa Rais wa Mpito wa Mali na Mahakama ya Kikatiba nchini humo, tarehe 28 Mei 2021.
Leave a comment