RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amesema mapendekezo ya kikosi kazi cha kukusanya na kuchakata maoni ya wadau wa demokrasia ya vyama vingi vya siasa “si amri kwa Serikali” licha ya kuahidi kwenda kuyafanyia kazi ndani ya Serikali. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Rais Samia ameeleza hayo leo Ijumaa, Oktoba 21, 2022 Ikulu jijini Dar es Salaam wakati akipokea mapendekezo ya ripoti ya kikosi cha kuratibu na kuchakata maoni ya wadau wa demokrasia kutoka kwa mwenyekiti Profesa Rwekaza Mukandala.
“Nimesikiliza vizuri uwasilishwaji uliofanywa na Profesa Mukandala na nimesikiliza vifungu vyote alivyovisema.Vingine nilikuwa nasema ilo kweli? Lakini ni maoni ya kikosi kazi,” amesema.
Hata hivyo amesema maoni hayo yatafanyiwa kazi ndani ya Serikali na kutaka pia kuwepo na nakala za kusambaza kwa wananchi ili wayaone licha ya kwamba maoni hayo si amri kwa Serikali.
“Maoni ya kikosi kazi si mwisho, si amri kwa Serikali kwamba lazima mfanye hivi kikosi kazi kimesema, tutaitana tena tuangalie hali halisi ndani ya Serikali lakini hali halisi ya Sheria zetu zingine ili tufanyie kazi vizuri,” amesema Rais Samia.
Ameongeza kuwa amepokea maoni yote ya marekebisho ya sheria na kwamba mapendekezo mengi ya kikosi kazi ni marekebisho ya sheria.
“Itabidi ndani ya Serikali tujipange vikosi kadhaa, wale watunga sheria, wale wa kuangalia mambo ya siasa na Katiba. Inabidi tujipange vikosi kadhaa ndani ya Serikali na pengine tuje tuwaombe tena baadhi yenu kuingia katika vikosi hivyo ili tuyafanyie kazi mlioyaleta.
“Kuna ambayo ni mepesi tunaweza kuyafanyia kazi haraka, lakini kuna ambayo lazima tukae na kuangalia sheria zilizopo zina mapungufu wapi? Na tunayabadilisha vipi kutokana na maoni yenu,” amesema Rais Samia.
Aidha amesema amepokea marekebisho ya vyama vya siasa na kuvitaka kujiangalia vyenyewe katika marekebisho hayo ikiwemo masuala ya jinsia, matumizi mazuri ya fedha na uendeshaji.
Amesema ni jambo zuri kwa vyama vya siasa kijiangalia vyenyewe lakini akasisitiza kuwa ni lazima kuwepo na taasisi nyingine ya kuviangalia na kusema kazi hiyo ni ya Msajili wa vyama vya siasa.
Leave a comment