RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, ametunukiwa Shahada ya Heshima ya Udaktari wa Falsafa (Doctorate Honoris Causa) na Chuo Kikuu cha Jawaharlal Nehru, nchini India. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ikulu ya Tanzania kupitia ukurasa wake wa Twitter, Rais Dk. Samia, ambaye yuko India kwa ziara ya kikazi, ametunukiwa shahada hiyo leo tarehe 10 Oktoba 2023 na Makamu Mkuu wa chuo hicho, Profesa Santishree Dhulipudi Pandit.
“Rais Samia ni mwanamke wa kwanza kutunukiwa shahada hiyo ya heshima na chuo hicho nchini India. Ni Viongozi wawili tu ambao wametunukiwa Shahada hiyo ya Heshima akiwemo Rais wa Urusi, Vladmir Putin pamoja na aliyekuwa Waziri Mkuu wa Japan Hayati Shinzo Abe,” imesema taarifa ya Ikulu.
Hafla ya tukio hilo imefanyika jijini New Delhi, nchini India na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali.
Akizungumza baada ya hafla hiyo, Rais Samia amewashukuru wazazi wake kwa kumsomesha, pamoja na familia yake kumruhusu kuendelea na masomo pamoja na shughuli za kisiasa ikiwemo uongozi serikalini, uliompeleka kutunukiwa shahada hiyo.
Hii shahada ya pili ya udaktari ambayo Rais Samia ametunukiwa, ya kwanza ikitoka katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), ikiwa ni sehemu ya kutambua mchango wake katika ujenzi wa taifa kupitia uongozi wake serikalini.
UDSM kilimtunuku shahada hiyo Rais Samia, mwishoni mwa 2022.
Leave a comment