RAIS Samia Suluhu Hassan amefanya teuzi na utenguzi wa viongozi mbalimbali, akiwemo aliyekuwa Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, ambaye amepelekwa kuwa Katibu Mkuu Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa ya teuzi hizo imetolewa leo tarehe 23 Septemba 2023 na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais-Ikulu, Zuhura Yunus.
Taarifa ya Yunus imesema kuwa, mrithi wa nafasi ya Mkurugenzi wa Idara ya Habari-Maelezo na Msemaji Mkuu wa Serikali, iliyokuwa inashikiliwa na Msigwa, atatangazwa baadae.
Kwa upande utenguzi, Rais Samia ametengua uteuzi wa aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Mtwara Mjini, Hanafi Msabaha na kumteua aliyewahi kuwa Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Mwanahamisi Mkunda, kushika wadhifa huo.
Rais Samia ametengua uteuzi wa aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu, Mariam Chaurembo, ambapo Dk. Stephen Mwakajumilo, ameteuliwa na Rais Samia kushika nafasi hiyo.
Pia, ametengua uteuzi wa Katibu Tawala Mkoa wa Mtwara, Mohamed Malela na kumteua Bahari Geuzye, kushika wadhifa huo.
Kiongozi mwingine aliyetenguliwa na Rais Samia ni aliyekuwa Mkurugenzi wa Mtwara DC, Tatu Issike na kumweka Abeid Abeid Kafunda.
Katika mabadiliko hayo, Rais Samia amemteua aliyekuwa Katibu Mkuu Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, Said Othman Yakubu, kuwa balozi.
Rais Samia amemteua aliyekuwa Mkurugenzi Msaidizi sehemu ya maafisa waandamizi Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Jumanne Gombati, kuwa Katibu Tawala Mkoa wa Geita.
Kwa mujibu wa taarifa ya Yunus, Rais Samia amemteua Dk. Erasmus Kipesha, kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA), awali alikuwa Mkurugenzi wa Huduma za Taasisi TEA.
Uteuzi na utenguzi wa viongozi hao umejiri siku kadhaa baada ya Rais Samia kufanya ziara ya kikazi katika mikoa ya kusini.
Leave a comment