DK. Bashiru Ally, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), ameapishwa rasmi kuwa Katibu Mkuu Kiongozi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Kwa mujibu wa televisheni ya taifa (TBC), Dk. Bashiru ameapishwa leo, Jumamosi, tarehe tarehe 27 Februari 2021, saa tatu asubuhi.
Dk. Bashiru aliteuliwa na Rais wa Tanzania, John Pombe Magufuli, kuwa Katibu Mkuu Kiongozi – Chief Secretary – jana Ijumaa, tarehe 26 Februari. Ameapishwa leo, Ikulu, jijini Dar es Salaam.
Hadi anateuliwa kushika wadhifa huo mkubwa katika utumishi wa umma na mpaka anapishwa leo, hakuna taarifa zozote zinazoonyesha kuwa Dk. Bashiru amejiuzulu nafasi yake ya ukatibu mkuu wa chama tawala.
Muda mfupi baada ya kuteuliwa kwake, kulisambaa kwenye mitandao ya kijamii, video inayomuonesha Dk. Bashiri “akijiapiza” kutokubali uteuzi mwingine wowote baada ya ule aliokuwa nao wa katibu mkuu wa CCM.
Katika video hiyo, Dk. Bashiru anasikika akisema, “cheo hiki ni kikubwa mno, na heshima hii niliyopewa ni kubwa mno. Ndio nafasi yangu kubwa ya kwanza na ya mwisho katika uongozi wa nchi hii.”
Aliongeza: “Sitagombea nafasi yoyote na sitakubali uteuzi wowote baada ya nafasi hii.” Wakati wote alipokuwa akizungumza matamtshi hayo, yalisikika makofi kutoka kwa wale aliokuwa akiwahubiria.
MwanaHALISI Online halikuweza kufahamu mara moja, Dk. Bashiru alitoa kauli hiyo lini na wapi. Haikuweza kufahamu pia nani hasa aliokuwa anawahutubia.
Hata hivyo, akizungumza baada ya kuapishwa na mbele ya Rais Magufuli, Dk. Bashiru amesema, taarifa za uteuzi wake alizipata kupitia mitandao ya kijamii.
“Jana jioni niko nasoma mafaili yangu, napata taarifa kupitia kwenye mitandao kwamba umeniteua. Mshtuko huo hauniwezeshi niseme, bado natafakari sana nitafanya nini. Nifanye nini kukidhi maratajio yako kwa imani uliyonipa mfululizo.”
Amemshukuru Rais Magufuli kwa kumwamini huku akimuahidi, kutomuangusha katika kazi aliyompa.
Alisema, “nakushukuru kwa imani yako kubwa, hii ni mara ya pili kwa kunipa wadhifa mkubwa; kwanza wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na sasa utendaji ndani ya serikali, imani hiyo nitailipa kwa imani.”
Kwa hiyo ile video ilikuwa feki au aliyoyasema yalikuwa feki?