MHADHIRI wa Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi (MUHAS), Profesa Deodatus Kakoko, ametoa wito kwa wananchi kuchanjwa chanjo ya Ugonjwa wa Corona (UVIKO-19), kwani haina madhara kama inavyodaiwa na baadhi ya watu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Prof. Kakoko ametoa wito huo leo Jumamosi, tarehe 27 Novemba 2021, akitoa mada katika semina ya wanahabari kuhusu afua za kinga dhidi ya tishi la wimbi la nne la UVIKO-19 na chanjo ya ugonjwa huo.
Iliyoandaliwa na Shirika linaloshughulika na masuala ya afya, Amref Health Africa Tanzania.
Prof. Kakoko amesema dhana inayodai kwamba chanjo hizo zinaathiri afya ya uzazi wa mwanamke na kusababisha tatizo la ugumba pamoja na kupunguza nguvu za kiume, si ya kweli.
“Lakini dhana juu afya ya uzazi na nafikiri liligusa pabaya kila mmoja anavyojua, sababu mara nyingi wote akili zetu ziko huko lazima tuwe na uhakika, imani imelezwa kuwa chanjo inaathiri uzazi wa wanawake wasizae, wawe wagumba na inaathiri nguvu za kiume,” amesema Prof. Kakoko.
Prof. Kakoko amesema “watu wengi wamekuwa wakikwepa lakini maneno hayo si kweli, uchunguzi wa kisayansi umeonesha hakuna kitakachochangia kupunguza nguvu za kiume na waelimishaji tumeenda kueleza jamii.”
Vile vile, Prof. Kakoko amewashauri wananchi waepukane na dhana potofu ya kwamba UVIKO-19 unawaathiri matajiri, wazee na watu waishio maeneo ya mjini peke yake, kwani siyo ya kweli kwa kuwa janga hilo linawathiri watu wote.
Mhadhiri huyo wa MUHAS amesema chanjo zilizoingiwa nchini zimefanyiwa uchunguzi na taasisi za Serikali, na kubainika kutokuwa na madhara.
Prof. Kakoko ametaja taasisi zilizofanya uchunguzi huo, ikiwemo Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA), Taasisi ya Taifa ya Utaiti wa Magonjwa ya Binadamu nchini (NIMR) na vyuo vikuu kadhaa.
“Sisi tulijihakikishia tunaziangalia, tunazikagua kuona kama zinafaa, kila chanjo hukagulwia taasisi za Serikali. Wamefanya kazi kubwa na taasisi zote zimechunguza, hii inatupa uhakika dhana hizi hazina ukweli wowote,” amesema Prof. Kakoko.
Leave a comment