SERIKALI ya Tanzania inatarajiwa kupewa msaada wa fedha kiasi cha Sh. 980 bilioni na Serikali ya Marekani, kwa ajili kuongeza nguvu katika mapambano ya kudhibiti Virusi vya Ukimwi (VVU) na Upungufu wa Kinga Mwilini (UKIMWI). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Hayo yalibainishwa jana Jumatatu na Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu, jijini Dar es Salaam, katika kikao cha kupitisha bajeti ya Mfuko wa Dharura wa Rais wa Marekani wa Kukabiliana na UKIMWI (PEPFAR), katika mwaka wa fedha wa 2024/2025.
“Tunaishukuru sana Serikali ya Marekani kwa kuendelea kuipatia Tanzania msaada kwa zaidi ya miaka 20 kwa ajili ya kupambana na VVU na UKIMWI, ambapo kwa sasa watatusaidia Bilioni 980 kwa ajili ya kupambana na ugonjwa huo,” alisema Ummy.
Ummy alisema fedha hizo zitasaidia katika utekelezaji wa mikakati ya kuyafikia makundi ambayo bado yana maambukizi mapya kwa kiwango kikubwa kama vile wasichana rika la balehe, wanawake vijana na vijana rika balehe na wanaume vijana.
Balozi wa Marekani Nchini Tanzania, Michael Battle ameipongeza Tanzania kwa kuendelea kufanya vizuri katika kufikia malengo katika kudhibiti maambukizi mapya na kutoa huduma za kufubaza virusi hivyo kwa waathirika.
Leave a comment