Jeshi la polisi mkoani Kilimanjaro limekamata shehena ya dawa za kulevya aina ya mirungi ndani ya basi la Extra Luxury lenye namba za usajili T643 DVL ikisafirishwa kutoka mkoani Arusha kwenda jijini Dar es salaam. Anaripoti Safina Sawart … (endelea).
Kamanda wa polisi mkoa wa Kilimanjaro, Simon Maigwa alithibitisha kukamatwa kwa basi hilo likiwa na shehena hiyo ya mirungi ambayo ni misokoto 365 sawa na kilogram 55 kiwango ambacho kinatajwa kuwa ni kikubwa.
Maigwa alisema kuwa gari hilo lilikamatwa tarehe 6 Desemba 6 mwaka huu, saa nne na nusu asubuhi, katika eneo la majengo mapya, Hedaru, Wilaya ya Same likitokea mkoani Arusha kwenda Dar es salaam.
Alisema kuwa, baada ya polisi waliokuwa doria kupata taarifa za gari hilo kuwa limebeba dawa hizo za kulevya lilipofika eneo la Majengo, wilayani Same walifanya upekuzi ndani ya gari hilo na kwenye buti walikuta dawa hizo za kulevya.
“Hili tukio lilitokea Desemba 6, majira ya saa nne na nusu, maeneo ya majengo mapya, Hedaru, barabara ya Tanga -Dar es salaam, kata ya Hedaru, tarafa ya Chome wilaya ya Same, polisi wetu waliokuwa doria walipata taarifa kwamba gari la Extra Luxury likiendeshwa na dereva(majina tunayahifadhi) lilikuwa limebeba dawa za kulevya,” alisema.
Alieleza kuwa basi hilo lilikamatwa wakati likisafirisha wanafunzi wa shule ya Arusha sayansi kutoka Jijini Arusha kuelekea Dar es salaam wakirejea kwenye familia zao baada ya muhula wa mwisho wa masomo kumalizika.
Alifafanua kuwa mirungi imeingizwa kwenye sheria ya dawa ya kulevya na mtu anayepatikana na hatia ya kusafrisha dawa hazo adhabu yake ni kifungo cha maisha jela huku anayekutwa akitumia adhabu yake ni kifungo cha miaka 30 jela.
“Kosa la kusafrisha dawa kulevya linaangukia kwenye kifungu cha 15 kifungu kidogo cha kwanza(b) cha sheria namba 5 ya mwaka 2015 ya udhibiti wa usafirishaji wa dawa za kulevya kama ilivyofanyiwa marejeo madogo ya sheria namba 23 ya mwaka 2016,” alisema.
Leave a comment