Kiongozi Mkuu wa Kanisa Katoliki Duniani, Baba Mtakatifu – Papa Francis amemualika Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kuitembelea Vatican tarehe 11 – 12 Februari 2024. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Hayo yamebainishwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, January Makamba alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari leo Jumapili Jijini Dar es Salaam.
Makamba ameeleza Rais Samia akiwa Vatican, atakuwa na mazungumzo na Baba Mtakatifu Papa Francis pamoja na Katibu wa Vatican, Pietro Parolin.
Amesema uhusiano kati ya Tanzania na Vatican ulianza miaka ya 1960 wakati ambapo Vatican ilianzisha Ubalozi wake hapa nchini.
Tangu wakati huo Vatican kupitia Kanisa Katoliki imekuwa mstari wa mbele katika kujishughulisha na masuala ya kiroho, amani, elimu na program za afya.
Kwenye ziara hiyo Rais Samia ataongozana na wawakilishi watano wa waumini wa Kanisa Katoliki Tanzania kutoka kwenye jumuiya mbalimbali za kanisa hilo.
“Vatican kupitia Kanisa Katoliki limechangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya sekta ya elimu kabla na baada ya uhuru wa Tanzania Bara kwa kutoa elimu kwa Watanzania wa dini zote. Kupitia shule na vyuo mbalimbali Kanisa kwa kushirikiana na Serikali limechangia kwa kiasi kikubwa kuzalisha viongozi na wataalam mahiri kwenye maeneo mbalimbali,” alieleza Makamba na kuongeza;
“Kanisa Katoliki linakadiriwa kumiliki zaidi ya shule za chekechea 240, shule za msingi 147, shule za sekondari 245, vyuo vya ufundi 110, vyuo vikuu 5 na taasisi za afya 473 zikiendeshwa na Kanisa Katoliki.”
Katika ziara hiyo Tanzania inaangalia fursa za kuanzisha maeneo mapya ya ushirikiano yatakayotoa msukumo mkubwa zaidi kwenye kuimarisha na kukuza amani na usalama.
Leave a comment