MAKAMO wa Kwanza wa Rais Visiwani, Othman Masoud Othman, ameonyesha kuwa ataendeleza kwa vitendo, matamanio na mwelekeo wa mtanguzi wake katika nafasi hiyo, Maalim Seif Sharif Hamad. Anaripoti Yusuph Katimba, Dar es Salaam … (endelea).
Akihutubia waamuni wa Kiislamu katika dua maalum ya kumuombea Maalim Seif, iliyofanyika jana mjini Unguja, Othman alitaka wananchi kumuunga mkono Rais wa Zanzibar, Dk. Hussein Ali Mwinyi, katika kutimiza wajibu wake.
Dua maalum ya kumuombea Maalim Seif, ilifanyika katika msikiti wa Muembe Tanga, Unguja. Ilihudhuriwa na maelfu ya wananchi, wakiwamo viongozi wa kiserikali.
Maalim Seif alifariki dunia, tarehe 17 Februari 20121, katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili, jijini Dar es Salaam. Alizikwa siku iliyofuata, Alhamisi ya tarehe 18 Februari, nyumbani kwake Mtabwe, mkoa wa Kaskazini Pemba.
Jabali hilo la kisiasa nchini, lilifikwa na mauti baada ya kuwa hospitali kwa takribani wiki tatu, kufuatia kupata maambuziki ya virusi vya Corona.
Othman aliapishwa kushika wadhifa wa Makamo wa Kwanza wa Rais, Jumatatu iliyopita.
“Ninaomba wananchi wa Zanzibar, kuachana na makandokando yaliyopita. Tushirikiane na Dk. Mwinyi kujenga umoja,” alieleza Makamo huyo wa Kwanza wa Rais Visiwani.
Alisema, kuna kila sababu ya kusonga mbele na mtazamo wa Maalim Seif” na kusisitiza, “Rais wa sasa, Dk. Mwinyi ana dhamira ya kweli ya kuleta umoja na maelewano Visiwani.”
Amesema, alimfahamu vizuri Maalim Seif na kwamba moja ya sifa yake, alikuwa muumini wa umoja.
Kutokana hilo, Othman akaomba wananchi kusimamia misingi hiyo, kwa kuwa watakuwa wanamuenzi jemedari huyo wa kisiasa za upinzani na haki.
Leave a comment