OFISI ya Msajili wa Vyama vya Siasa ameagiza watu wanaofanya siasa kwa kutumia jina la Chama cha Umoja Party, kuacha kufanya shughuli hizo kwa kuwa chama hicho hakijasajiliwa licha ya kuwasilisha maombi ya kupata usajili wa muda. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Onyo hilo limetolewa leo Jumanne, tarehe 19 Aprili 2022 na Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa, Sisty Nyahoza, baada ya kusambaa kwa picha za baadhi ya watu waliovaa fulana zenye jina la Umoja Party na picha ya aliyekuwa Rais wa Tanzania, Hayati John Magufuli.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Nyahoza amewataka waanzilishi wa chama hicho kusuburi majibu ya maombi yao ya usajili.
“Mtu yeyote anayefanya siasa kwa kutumia jina Umoja Party, bendera, nembo au alama yoyote ya chama hicho, anakiuka sheria na anapaswa kuacha mara moja.
“Aidha, waanzilishi wa chama hicho wanashauriwa kuendelea kufuatilia maombi ya usajili wa muda waliyowasilisha,” imesema taarifa ya Nyahoza.
Taarifa ya Nyahoza imewaonya wanachama wa chama hicho, kuacha kutumia fulana zilizowekwa picha ya kiongozi ambaye sio mwanachama wake.
“Ofisi ya Msajili inatumia fursa hii kuwakumbusha wanaotengeneza, wanaovaa fulana hizo na Watanzania wote kwa ujumla kuwa, ni kosa la kisheria kwa taasisi yoyote kufanya kazi kama chama cha siasa wakati siyo kilichosajiliwa.
“Ni kosa chama cha siasa kilichowasilkisha maombi ya usajili wa muda, kufanya kazi kama chama cha siasa wakati hakijapewa cheti cha usajili wa muda,” imesema taarifa ya Nyahoza na kuongeza:
“Kifungu husika cha Sheria ya Vyama vya Siasa, sura ya 258, kinaeleza hakuna taasisi itakayoendeshwa au kufanya kazi kama chama cha siasa isipokuwa kusajiliwa kwanza kwa mujibu wa kifungu cha sheria hii.”
Leave a comment