MKURUGENZI Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Bernard Konga amesema watoto wote wanaotumia Toto Afya Kadi hivi sasa na wale waliokwisha kulipia huduma hiyo wataendelea kupata matibabu na pale bima zao zitakapoisha watalazimika kujisajili kwa utaratibu mpya. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Amesema kuwa hakutakuwa tena na usajili wa Toto Afya Kadi bali wazazi na walezi wanashauriwa kuandikisha watoto kama tegemezi kupitia bima zao kwa mwajiri au vifirushi vya watu ama kuwasajili kupitia shule wanazosoma.
Akizungumza mbele ya waandishi wa habari leo Jumanne tarehe 14 Machi 2023 Jijini Dodoma, ikiwa ni siku moja tangu kutolewa kwa tangazo la kufanyika kwa maboresho katika utaratibu wa usajili wa watoto, Konga ametolea ufafanuzi baadhi ya masuala ambayo yameanza kuibua sintofahamu.
“Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) unapenda kutangazia Umma kuwa unafanya maboresho ya utaratibu wa usajili wa huduma kwa watoto waliokuwa wansajiliwa kupitia utaratibu wa bima ya afya ya Toto Afya Kadi kwa sasa wazazi au walezi wanashauriwa kuwasajili watoto wao kama wategemezi wao kwenye bima ya afya au kuwasajili kupitia shule wanazosoma,” lilisomeka tangazo hilo kwa umma.
“Lengo ni kuongeza wigo wa wananchama katika makundi yao wanajiunga kama familia au kaya au makundi ya wanafunzi kupitia shule wanazosoma.”
Akitoa ufafanuzi kuhusu malalamiko juu ya watoto ambao hawajaanza shule ambao wapo chini ya miaka mitano amesema watatumia manufaa ya Sera ya Serikali kutoa matibabu bure kwa watoto wa umri huo katika vituo vya afya vya serikali.
Ametaja manufaa ya utaratibu huo mpya kuwa umepunguza pia muda wa kusubiri kupata huduma ambapo kwa watakaosajili kupitia taasisi za elimu wataanza kupata huduma mara moja badala ya siku 90.
Amesema kwa wale watakaosajiliwa kama wategemezi wa vifurushi vya wazazi wao wataanza kupata huduma baada ya siku 30.
Amesema kuwa utaratibu huo unalenga kusajili watoto na wazazi wengi zaidi ikiwa ni hatua ya kuelekea katika mpango wa Serikali wa bima ya Afya kwa wote.
Leave a comment