KATIBU mkuu wa CCM, Balozi Dk. Emanuel Nchimbi amesema mbali na kumpoteza rafiki, na kaka, pia Taifa na Afrika imempoteza Mwana Afrika ukweli kutokana na kifo cha aliyekuwa waziri mkuu mstaafu wa Tanzania, Edward Lowassa.
Dk. Nchimbi ametoa kauli hiyo leo Ijumaa nyumbani kwa Lowassa katika kijiji cha Ngarash – Monduli mkoani Arusha kushiriki na waombolezaji kuaga mwili wa kiongozi huyo anayetarajiwa kuzikwa kesho Jumamosi.
Amesema pia vyama vya siasa vimepoteza mtu wa karibu na ni pigo kubwa kwa nchi yetu.
“Lowasa alikuwa Mwana Afrika wa ukweli na mchapakazi… watu wanaweza kupishana katika maelezo yote kumhusu yeye lakini hakuna anayeweza kusema hakuwa mchapakazi.
“Lowassa alikuwa mnyeyekevu anayejali marafiki wote, alikuwa haangalii nafasi zao. Hata watu wa kawaida alikuwa anawajali ndio maana wamekuja kumuaga. Alikuwa hachagui marafiki na hili ametuachia funzo kwetu kuwa na upendo kwa wote,” amesema.
Aidha, Nchimbi amesema atamkumbuka Lowassa kwa namna mbalimbali kwa sababu pia yeye pia ana ugonjwa wa kupenda watu wachapakazi wa kweli.
“Ninawapenda wanaopenda nchi kwa dhati na haya ni mambo ya pekee nitayakumbuka na kuendelea kuyaenzi. Mapenzi yake hayakuchagua itikadi yoyote. Alikuwa habagui wala kuchagua hakika ni afya kwa nchi yetu,” amesema Dk. Nchimbi.
Leave a comment