MWALIMU wa Shule ya Msingi Global International School iliyipo Vijana Wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam, Daniel Chacha Magere (26) amefikishwa Mahakama ya Wilaya ya Kinondoni kwa tuhuma za kuwabaka, kuwalawiti na kuwashambulia kwa aibu baadhi ya wanafunzi anaowafundisha. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Mwalimu huyo amepandishwa leo Jumanne tarehe 31 Mei 2022 mbele ya Mahakimu tofauti akikabiliwa na mashtaka sita ya ubakaji kwa watoto watatu wenye umri tofauti ikiwemo wa miaka saba.
Mwendesha Mashtaka wa Wakili wa Serikali, Hilda Kato amedai mbele ya Hakimu Mkazi, Frankoo Kiswaga kuwa mtuhumiwa kwa nyakati tofauti Januari na Mei 2022 akiwa shuleni kwake aliwabaka na kulawiti wanafunzi wake wa kike (majina yamehifadhiwa) kinyume na sheria.
Aidha, Mwendesha Mashtaka Wakili wa Serikali, Daisy Makalala amedai mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama hiyo, Aron Lyamuya kuwa mtuhumiwa akiwa kazini kwake alimlazimisha mwanafunzi wake wa kike kumnyonya sehemu zake za siri kwa lengo kujiridhisha kingono.
Shtaka lingine ni kumdhalilisha kingono mwanafunzi wake ambapo Mwendesha Mashtaka, Daisy Makalala amedai katika tarehe hizo Mwalimu huyo mkazi wa Mwananyamala A akiwa shuleni kwake aliviingiza vidole vyake sehemu za siri za mwanafunzi wake wa kike (jina linahifadhiwa) kwa lengo la kujiridhisha kingono.
Mtuhumiwa amekana tuhuma zinazomkabili na amepelekwa rumande baada ya upande wa mashitaka kuweka kiapo cha kupinga dhamana.
Upelelezi wa kesi hizo umekamilika na kuahirishwa mpaka tarehe 13 Juni 2022 ambapo yataanza kusomwa maelezo ya awali.
Leave a comment