RAIS wa Uganda, Yoweri Museveni, amesema maradhi ya Uviko-19 na Vita vya Ukraine na Urusi ni fursa kwa nchi za Afrika. Anaripoti Mwandishi Wetu Arusha … (endelea)
Rais huyo anayeiongoza Uganda kwa muda mrefu sasa amesema kutokana na Uviko-19 Uganda imeendeleza tafiti zao za kutengeneza chanjo ya maradhi hayo pamoja na maradhi mengine.
Ametoa kauli hiyo leo Alhamis Tarehe 21 Julai, 2022, kwenye mkutano wa kawaida wa wakuu wa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashiriki unaofanyika jijini Arusha.
Amesema badala ya kufungasha chanjo ambazo zimetngenezwa nje, wao wanataka kutengeneza kuanzia mwanzo hadi kufungasha.
Pia amesema Uganda inatengeneza magari ya umeme ambayo uendeshaji wake ni wa gharama nafuu ikilinganishwa na bei ya mafuta ambayo imepanda sana.
Amesema wanaendelea kuboresha magari hayo ili yaweze kupata soko kubwa nje ya Uganda na kusisitiza nchi za Afrika kutumia rasilimali zake kutengeneza bidhaa badala ya kutegemea bidhaa kutoka nje.
Katika hatua nyingine amesema sera za nchi za EAC zinaweza kuwa kikwazo cha mandeleo ya nchi hizo kwa kuminya ukubwa wa soko ambalo lipo.
Museveni amesema ni vyema kuwa na soko huru ili kuwezesha bidhaa zao kupata soko kubwa na kila nchi kubobea kwenye mazao ambayo yanastawi kwa urahisi.
Leave a comment