LUTENI Jenerali, Muhoozi Kainerugaba, mtoto wa Rais wa Uganda, Yoweri Museveni, amesema baba yake ameruhusu kufanyika kwa kongamano la vijana wazalendo, lenye lengo la kujadili namna ya kufanya mapinduzi nchini humo. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Jenerali Kainerugaba ametoa taarifa hiyo jana Alhamisi, katika ukurasa wake wa Twitter, huku akiwaalika viongozi mbalimbali wa kimataifa, kushiriki kongamano hilo, huku akisema Mwenyekiti wa kongamano hilo atakuwa Rais wa China, Xi Jinping.
“Kama Amiri Jeshi Mkuu wa Jeshi la MK, nina furaha kutangaza kwamba kamanda wetu mkuu wa mapinduzi, Kaguta Museveni, ameturuhusu kuwa na kongamano la vijana wazalendo katika wiki chache zijazo. Itakuwa wakati mzuri wa kujadiliana,” aliandika mtoto huyo wa Rais Museveni.
Jenerali Kainerugaba aliandika “tutakuwa na wasemaji wa kigeni kutoka kote ulimwenguni. Tunajitahidi kupata ulimwengu bora. Mapinduzi ya Uganda chini ya uongozi wa kamanda wetu wa milele wa Kaguta Museveni utatoa majibu kwa kizazi kipya.”
Kupitia ukurasa wake huo wa Twitter, Jenerali Kainerugaba aliwaalika baadhi ya viongozi wa kimataifa kushiriki kongamano hilo, akiwemo Rais wa Urusi, Vladimir Putin na Rais wa Marekani, Joe Biden, aliyewataja kama mabosi wawili.
Amongst our elders…We invite H.E. General Yoweri Museveni, H.E. General Paul Kagame, H.E Ramaphosa, H.E. Jacob Zuma, Her Excellency President Samia Suluhu Hassan of Tanzania, H.E. General Buhari, H.E. Field Marshal Abdel Fattah El-Sisi…more names to follow.
— Muhoozi Kainerugaba (@mkainerugaba) October 27, 2022
Wengine ni, Rais wa Rwanda, Paul Kagame. Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan. Rais wa Burundi, Evariste Ndayashimiye. Rais wa Demokrasia ya Congo, Felix Tshishekedi na kiongozi wa upinzani nchini Afrika Kusini, Julius Malema.
Mara kwa mara kupitia ukurasa wake wa Twitter, Jenerali Kainerugaba amekuwa akitoa wito kwa vijana wa nchi za Afrika Mashariki kaunzisha vuguvugu la kuunganisha nchi za jumuiya hiyo ili ziweze kuwa na nguvu na kupata maendeleo.
Aliandika akisema atatembea kutoka Uganda kwenda katika nchi hizo ikiwemo katika Jiji la Dar es Salaam , Tanzania, kuhamasisha suala hilo.
Mtoto huyo wa Rais wa Uganda, amejizolea umaarufu katika mtandao wa Twitter kupitia maandiko mbalimbali anayoyatoa ikiwemo lile lililosema ataliteka Jiji la Nairobi nchini Kenya kwa muda wa wiki mbili.
Leave a comment