MSEMAJI Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, amesema mchakato wa marekebisho ya sheria za habari unakwenda vizuri na kwamba hivi karibuni Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye, atakutana na wadau kwa ajili ya kupitia mapendekezo yaliyotolewa kuhusu suala hilo. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Akihojiwa na kituo cha televisheni cha ITV, leo Ijumaa, tarehe 28 Oktoba 2022, jijini Dar es Salaam, Msigwa amesema kazi iliyobakia katika mchakato huo ni ndogo kwani kila kitu kimeshafanyika.
“Nafurahi kwamba mchakato unakwenda vizuri, tumeshakutana na wadau tumepokea maoni yao, maoni ya Serikali pia yamekusanywa na sasa kinachoandaliwa ni mkutano ambao utamkutanisha waziri na wadau, tutautangaza wakati wowote lini tunaufanya,” amesema Msigwa.
Msigwa amesema “ lengo ni kuhakikisha kwamba kama kuna mabadiliko tutayafanya kwenye sheria yawe yamezingatia maoni ya wadau wote, lisiwe jambo la mtu mmoja au taasisi moja au chombo fulani. Liwe jambo la sekta nzima ya habari ili tunapotoka tuwe na sheria ambayo wote tutaiona muongozo.”
Msigwa amesema marekebisho ya sheria hususan Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari ya 2016, ni sehemu ya eneo ambalo Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan, imeamua kufanyika kazi ili kuimarisha na kukuza zaidi uhuru wa vyombo vya habari, kutengeneza mazingira bora ya sekta hiyo.
Aidha, Msemaji huyo wa Serikali ya Tanzania, amesema mchakato huo umechelewa kwa sababu wadau waliongezewa muda wa kuwasilisha mapendekezo yao.
“Mchakato umechelewa kwa sababu lazima tushirikishe wadau wote, huwezi kuwapata kwa siku moja. Kwanza tulikutana na wadau kutoka serikalini, taasisi mbalimbali, vyombo vya habari na mashirika. Tumeyakusanya tukaenda kifungu kwa kifungu, kipi kibadilishwe kipi kiachwe,” amesema Msigwa na kuongeza:
“Sasa hivi waziri atakutana na wadau wote, sheria hii itafanyiwa marekebisho palipobaki ni padogo sana na karibu kila kitu kimeshafanyika.”
Miongoni mwa sheria ambazo wadau wa habari wamependekeza zifanyiwe marekebisho ili kuondoa vifungu kandamizi kwa uhuru wa habari ni, Sheria za Huduma za Vyombo vya Habari ya 2016, Sheria ya Makosa ya Mtandaoni ya 2015, Sheria ya Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta (EPOCA), Sheria ya Haki ya Kupata Taarifa ya 2016 iliyofanyiwa marekebisho 2017 na Sheria ya Takwimu.
Baadhi ya vifungu vinavyolalamikiwa ni vile vinavyotoa mamlaka kwa watendaji wa Serikali dhidi ya vyombo vya habari hususan katika masuala ya utoaji leseni, adhabu, matangazo na tafsiri ya mwandishi wa habari.
Leave a comment