JENERALI Brice Nguema, aliyemng’oa madarakani Rais wa Gabon, Ali Bongo katika mapinduzi ya kijeshi yaliyofanyika wiki iliyopita, ameapishwa kuwa Rais wa mpito wa nchi hiyo kwa kipindi kisichojulikana. Anaripoti Isaya Temu, TUDARCo…(endelea).
Jenerali Nguema, amekula kiapo katika ikulu ya Rais leo tarehe 4 Septemba 2023, mbele ya chumba cha maafisa wa serikali, jeshi na viongozi wa eneo hilo katika mji mkuu wa Gabon, Libreville.
Hayo yamejiri ikiwa ni wiki moja imepita baada ya Mapinduzi yaliyomngoa madarakani Rais Ali Bongo Odimba akiwa ni mmoja wa wanafamilia waliodumu madarakani kwa miaka 55.
“Naapa mbele za Mungu na watu wa Gabon kuulinda utawala wa Jamhuri kwa uaminifu,” ameapa Nguema.
Akizungumza na waandishi wa habari baada ya uapisho, Oligui amesema jeshi limechukua madaraka bila umwagaji damu na kuahidi kurejesha madaraka kwa wananchi kwa kuandaa uchaguzi huru, wa uwazi na wa kuaminika.
“Kwa serikali mpya, iliyoundwa na watu wenye uzoefu, tutampa kila mtu nafasi ya matumaini,” amesema.
Televisheni ya taifa ilionyesha picha za umati wa watu waliokuwa wakishangilia na vifaru vya Majeshi wakifyatua risasi baharini kuashiria furaha ya tukio hilo.
Hata hivyo pamoja na kutwaliwa kwa madaraka na Jeshi nchini Gabon bado kutasababisha kuendelea kwa utawala wa ukoo wa Bongo ambao umekuwa madarakani kwa miaka 55, chanzo kilicho karibu na Rais aliyeondolewa madarakani kimesema.
“Jenerali Brice Oligui Nguema ni zao la moja kwa moja la ukoo wa Bongo,” kilisema chanzo hicho, ambacho kilitaka kubaki bila kujulikana kwa sababu za kiusalama.
Jeshi nchini Gabon lilitangaza kuchukua madaraka hayo ya Urais muda mfupi baada ya Rais Ali Bongo kutangazwa mshindi wa uchaguzi uliokumbwa na utata.
Rais aliyepinduliwa bado yuko nyumbani kwake baada ya kuwekwa kizuizini na Jeshi wakati walipotwaa madaraka yake huku baadhi ya ndugu zake walikamatwa na uchunguzi unaendelea nchini Gabon pamoja na Ufaransa walipokimbilia baada ya mapinduzi.
Leave a comment