MBUNGE wa Kisesa, Luhaga Mpina, amehoji bungeni jijini Dodoma, sababu za mchakato wa marekebisho ya katiba, kukwama licha ya Rais Samia Suluhu Hassan, kuagiza ufufuliwe. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Mpina amehoji hayo leo tarehe 8 Februari 2023, akidai kwamba hadi sasa hakuna muongozo wowote wa marekebisho ya Katiba hiyo.
“Rais wetu alitoa muongozo kuanzia Juni 2022 kuhusiana na kuanza mchakato wa maandalizi ya marekebisho ya katiba tuliyo nayo, lakini pia hata mapendekezo ya katiba mpya. Lakini mpaka sasa hivi Wizara ya Katiba na Sheria hakuna muongozo wowote, hakuna deadline yeyote, utafiti wowote na hakuna jambo hili,” amesema Mpina.
Mpina amesema “mpaka sasa hivi toka kiongozi wa nchi atoe maelekezo leo ni miezi saba, halijawekwa mahala popote, kwa hiyo huwezi kuona linafanyiwa kazi namna gani.”
Mbunge huyo wa Kisesa amesema kuwa, ni muda muafaka wa kurekebisha katiba iliyopo akidai ina mapungufu yanayopelekea ubadhirifu wa fedha za Serikali.
“Ni muda muafaka wa kuangalia katiba yetu na moja ya eneo ambalo ni muhimu sana ni kwamba, katiba tuliyonayo haina nguvu ya kutosha kulinda na kusimamia fedha na rasilimali za umma. Kwa sasa ndiyo maana wabunge walivyokuwa wakichangia kamati za kifedha wote wamelalamika fedha zimeibiwa,” amesema Mpina na kuongeza:
“Taarifa za CAG (Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali), taarifa ya Taasisi na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), zote watu wanalalamika wizi wa fedha, lakini wizi wa fedha ambao hauna dawa inawezekana kuna tobo kubwa liko kwenye katiba ndiyo maana hatujaweza tatua tatizo hili.”
Leave a comment