JESHI la Polisi mkoani Mwanza, linawashikiliwa watu wawili kwa tuhuma za kuongoza vurugu zinazodaiwa kufanywa na baadhi ya wafanyabiashara wadogo (wamachinga), dhidi ya askari mgambo wakipinga kuondolewa katika maeneo waliyokuwa wanafanya biashara. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mwanza … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo tarehe 8 Februari 2023 na Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza, SACP Wilbroad Mutafungwa, saa kadhaa baada ya vurugu hizo kutokea maeneo ya Makorobi, wilayani Nyamagana.
Kamanda Mutafungwa amesema kuwa, juhudi za kuwatafuta watuhumiwa wengine waliohusika na matukio hayo, zinaendelea kufanyika.
Akizungumzia athari za tukio hilo, Kamanda Mutafungwa amesema hakuna binadamu aliyeathirika isipokuwa magari mawili yaliahiribiwa kwa mawe yaliyokuwa yanarushwa na wamachinga.
“Bado tunafuatilia vijana wadogo ambao wahalifu walioshirikiana na machinga wakaongeza kundi kubwa wakarusha mawe. Waliokamatwa wanaendelea kuhojiwa ili hatua za kisheria zichukuliwe,” amesema Kamanda Mutafungwa.
Kamanda Mutafungwa amesema, fujo hizo zilianza majira ya saa 3.00 asubuhi katika Mtaa wa Makoroboi na Mtaa wa Lumumba, jijini humo, baada ya askari wa mgambo ambao wanafanya kazi chini ya uongozi wa Jiji la Mwanza, kufanya operesheni ya kuwazuia wamachinga kufanya biashara katika maeneo ambayo hayaruhusiwi.
Leave a comment