KIJANA mmoja anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 20 amewashambulia watu 14 kwa kuwagonga na gari na kuwachoma kwa kutumia kitu chenye ncha kali na kusababishia kifo na majeraha katika jiji la Seongnam karibu na mji mkuu Seol nchini Korea Kusini. Anaripoti Isaya Temu, TUDARCo … (endelea).
Mshukiwa huyo aliendesha gari lake hovyo na kuwagonga watu watano, kisha alishuka na kuwachoma visu watu wengine tisa katika kituo cha ununuzi chenye shughuli nyingi ambapo mwanaume mmoja anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 60 akifariki dunia baada ya shambulio hilo.
Mashuhuda wa tukio hilo, wameeleza kuwa walimuona kijana huyo akiwa amevalia mavazi yote meusi pamoja na miwani nyeusi huku akiwa amebeba kisu mkononi mwake na ndicho alichotumia kuwashambulia wahanga baada ya kushuka kwenye gari.
“Ghafla, mtu mmoja alituambia kwamba mtu aliyetenda kosa alikuwa akija kwenye ghorofa ya pili, hivyo tukakimbia kwa hofu,” alieleza shuhuda wa shambulizi hilo huku akiongeza kuwa baada ya taarifa hiyo watu wengine walijificha katika jokofu kwa hofu.
Polisi wa eneo hilo walifanya jitihada na kufanikiwa kumkamata kijana huyo dakika 10 baada ya taarifa kusambazwa na uchunguzi juu ya tukio hilo unaendelea.
“Watu tisa walichomwa kisu katika eneo hilo, huku wengine watano wakijeruhiwa baada ya mshukiwa kuendesha gari kwenye njia ya watembea kwa miguu kabla ya shambulio la kisu”, alisema Lee Ki-in, afisa wa serikali ya Mkoa wa Gyeonggi, katika taarifa kwenye Facebook.
Majeruhi wa tukio hilo walikimbizwa hospitalini kwa ajili ya matibabu ya haraka kwani wengi wa majeruhi walikuwa na hali mbaya.
Viongozi walijadili kuongeza doria za usiku katika maeneo ya starehe na mengine yenye watu wengi na kuimarisha ufuatiliaji wa kamera za usalama.
Mwezi uliopita, mtu aliyekuwa na visu aliwadunga kisu angalau watembea kwa miguu wanne kwenye barabara katika mji mkuu Seoul.
Leave a comment