SERIKALI ya Tanzania imewasilisha na kusoma mara ya kwanza miswada ya sheria mbalimbali, ikiwemo Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote na Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi ambayo ni miongoni mwa miswada inayosubiriwa kwa hamu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Miswada hiyo umewasilishwa na kusomwa kwa mara ya kwanza leo Ijumaa, tarehe 23 Septemba 2022, bungeni jijini Dodoma.
Kuhusu Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote, katibu wa Bunge amesema umewasilishwa kwa ajili ya kuweka mfumo bora wa bima ya afya kwa wote.
“Muswada wa sheria ya bima ya afya kwa wote, kwa ajili ya kuweka mfumo bora wa bima ya afya kwa wote, kuimarisha mfumo wa afya kupitia bima ya afya kwa wote, kuweka masharti ya kupanua wigo wa huduma ya afya,” amesema katibu wa Bunge.
Muswada mwingine uliowasilishwa bungeni ni, wa Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi, wenye lengo la kuweka misingi ya ulinzi wa taarifa binafsi.
“Muswada wa sheria ya ulinzi wa taarifa binafsi kwa lengo la kuweka misingi ya ulinzi wa taarifa binafsi, kuweka kiwango cha chini cha matakwa ya ukusanyaji na uchakataji wa taarifa binafsi, kuanzisha tume ya ulinzi wa taarifa binafsi na kuimarisha ulinzi wa taarifa binafsi zinazochakatwa na vyombo vya Serikali na binafsi, pamoja na masuala mengine yanayohusiana na hayo,” amesema Katibu wa Bunge.
Muswada mwingine uliosomwa ni ule wa kufanyia marekebisho Sheria mbalimbali saba kwa lengo la kufanya marekebisho changamoto zilizoibuka katika utekelezaji wa sheria hizo.
Baada ya miswada hiyo kusomwa kwa mara ya kwanza, Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson, amesema itawasilishwa katika kamati za Bunge husika kwa ajili ya kufanyiwa kazi.
“Miswada minne imesomwa hapa kwa mara ya kwanza na kwa utaratibu wetu miswada hii itaelekezwa kwenye kamati zinazohusika na watakapokamilisha kazi watanitaarufu halafu italetwa hapa bungeni ili Bunge tuweze kujadili na kuweza kutunga sheria,” amesema Spika Tulia.
Leave a comment