SERIKALI ya Tanzania imewasilisha Muswada wa Sheria ya Uwekezaji, uliosomwa kwa mara ya kwanza Bungeni wenye malengo mbalimbali ikiwemo kufuta Sheria ya Uwekezaji Tanzania ya 1997. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Muswada huo pamoja na miswada mingine, imewasilishwa na kusomwa kwa mara ya kwanza leo Ijumaa, tarehe 23 Septemba 2022, bungeni jijini Dodoma.
Akisoma muswada huo, Katibu wa Bunge, amesema una lengo la kuweka mazingira bora kwa wawekezaji, kuweka mfumo wa kitaasisi kwa ajili ya utaratibu na usimamizi wa uwekezaji nchini.
“Muswada wa Sheria ya Uwekezaji kwa lengo la kuweka mazingira bora kwa wawekezaji, kuweka mfumo wa kitaasisi kwa ajili ya utaratibu na usimamizi wa uwekezaji nchini, kufuta sheria ya uwekezaji Tanzania ya 1997, pamoja na masuala mengine yanayohusiana na hayo,” amesema Katibu wa Bunge.
Baada ya muswada huo kusomwa kwa mara ya kwanza, Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson, amesema utapelekwa katika kamati husika ya mhimili huo kwa ajili ya kufanyiwa kazi kisha utaletwa bungeni kwa ajili ya kujadiliwa na kupitishwa.
Leave a comment