RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, amewahamisha waliokuwa vigogo wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), katika kipindi ambacho kuna changamoto ya ratiba ya upatikanaji nishati hiyo nchini. Anaripoti Matilda Peter, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais-Ikulu, Zuhra Yunus, imesema leo tarehe 23 Septemba 2023, Rais Samia amemteua Jenerali Paul Kisesa Simuli, kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TANESCO, akichukua nafasi ya Omar Issa, aliyepangiwa majukumu mengine katika Ofisi ya Rais-Tume ya Mipango.
Kigogo mwingine aliyeondolewa TANESCO ni aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa shirika hilo, Maharagande Chande, ambaye Rais Samia amemteua kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL).
Rais Samia amemteua Mhandisi Gissima Nyamo-Hanga, kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO. Kabla ya uteuzi huo, Mhandisi Nyamo-Hanga aliwahi kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA).
Mabadiliko hayo yamefanywa na Rais Samia , baada ya wananchi kuibua vilio vyao juu ya changamoto ya kukatika kwa umeme, ikiwemo athari wanazopata kiuchumi.
Akitangaza ratiba ya upatikanaji wa umeme, Chande alidai hatua hiyo inajiri kutokana na upungufu wa uzalishaji wake.
Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dotto Biteko, alisema serikali inachukua hatua za haraka kutafuta Suluhu ya changamoto hiyo.
Leave a comment