MBUNGE wa zamani wa viti maalum kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Upendo Peneza, amejiunga rasmi na Cha Mapinduzi (CCM), akidai chama chake cha zamani hakipo kwa ajili ya kuwatafutia mabadiliko wananchi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Peneza ametangaza uamuzi wake huo leo tarehe 22 Januari 2024, alipokaribishwa katika mkutano wa kumkaribisha katibu mkuu mpya wa CCM, Dk. Emmanuel Nchimbi, jijini Dodoma.
“Wikiend hii nimekuwa na tafakari ya muda mrefu sana, safari hii haijaanza ndani ya wiki moja imeanza muda mrefu sana nikafanya mawasiliano na viongozi na hatimaye wakakubali kunipokea. Napenda kumshukuru Mungu kwa miaka 15 aliyonipa nikiwa chama cha upinzani na kumuomba anipe nguvu, ustahimilivu, hekima, busara na nguvu za kutumika kwenye chama change kipya,” amesema Peneza.
Peneza amedai uamuzi wake wa kwenda CCM unatokana na Chadema kutoonesha nia ya kuleta mabadiliko kwa watanzania.
Pia, amedai uamuzi wake huo unatokana na kuridhishwa na utendaji wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, kuimarisha maridhiano, utawala bora na demokrasia ya vyama vingi.
“Katika safari hiyo niliyoanza miaka 15 iliyopita nilitamani kuona Tanzania yetu ikibadilika, ikiwa bora lakini leo nikiwauliza nyie wana CCM mliopo hapa kwa kweli kabisa bila ushabiki Chadema mnatuelewa kweli? Kweli tupo kwa ajili ya kutafuta mabadiliko ya wananchi?” amesema Peneza.
Leave a comment