MBUNGE Viti Maalum mkoani Tanga (CCM), Mwantum Zodo, ameiomba Serikali irejeshe mikopo inayotolewa na halmashauri kwa makundi maalum hususan wanawake, ili kuepusha na uchukuaji mikopo yenye masharti kandamizi maarufu kama kausha damu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Zodo ametoa ombi hilo leo tarehe 2 Februari 2024, katika kipindi cha maswali na majibu, bungeni jijini Dodoma.
“Kwa kuwa mchakato huu wa utoaji mikopo ya asilimia 10 ya fedha za halmashauri imesitishwa kwa muda mrefu sasa na kwa kuwa kina mama bado wanahangaika na mikopo ya kausha damu huko mitaani, lini Serikali itaanza tena zoezi la utoaji mikopo hiyo ili kuondoa adha ya kina mama?” amesema Zodo na kuongeza:
“Kwa kuwa halmashauri inatenga mikopo kwa kila robo ya mwaka, serikali ihakikishe kila halmashauri zinaendelea kutenga hizo asilimia 10 ili ukianza mchakato huu kina mama waendelee kupata mikopo?”
Naibu Waziri Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Deogratius Ndejembi, amesema mikopo hiyo ilisimamishwa kwa agizo kwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, baada ya ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), kubaini kwamba kuna ubadhirifu.
Amesema kufuatia agizo hilo TAMISEMI iliunda timu kwa ajili ya kufanya mapitio juu ya namna inavyotolewa kwa ajili ya kutafuta mwarobaini wa upotevu wa fedha, ikishamaliza mikopo hiyo itaendelea kutolewa kwa utaratibu maalum.
Leave a comment