MBUNGE wa Momba (CCM), Condester Sichalwe, ameichongea Wizara ya Maji kwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, akidai imeshindwa kutekeleza agizo lake la kutatua changamoto ya maji kwa wananchi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Sichalwe ametoa madai hayo leo tarehe 2 Februari 2024, bungeni jijini Dodoma, ambapo alimkabidhi Spika Tulia Ackson, video fupi inayoonyesha wananchi wakichota maji ya visima ambayo sio safi na salama kwa ajili ya matumizi ya binadamu.
“Mama yetu mpendwa ana kauli yake ya kumtua ndoo mwanamke kichwani lakini Wizara ya Maji ndani ya Momba imepinga kauli hii kwa vitendo, imekataa kabisa hiyo kauli. Leo nimekuja na clip kwenye simu yangu naomba uletewe mbele kama spika wetu ili uone kama maji haya wana Momba wanatumia binadamu wa kawaida anafaa kutumia,” amesema Sichalwe.
Sichalwe amesema “Juni 2023 ulinipa nafasi kusimama hapa kuomba mwongozo wa kuchimbiwa visima vya dharura, mpaka leo licha ya wananchi kuteseka hakuna hata tone la maji. Nikienda kwa wananchi naonekana tapeli.”
Baada ya Sichalwe kutoa malalamiko hayo, Waziri wa Maji, Jumaa Aweso alisimama bungeni kwa ajili ya kutoa ufafanuzi na kusema wizara yake imechukua hatua mbalimbali kutatua changamoto hiyo ikiwemo yeye binafsi kufika jimboni hapo.
“Nilipopata malalamiko ya mbunge nilifika jimboni kwake na ipo miradi inayoendelea kwa udharura. Nilitoa Sh. 1 bilioni kuhakikisha tunasapoti miradi. Niombe wabunge wakati mwingine tunaweza kuwakatisha tamaa wanaofanya kazi kubwa. Nimhakikishie mbunge sisi hatutakuwa kikwazo kwa wananchi wa Momba kupata maji safi na salama,” amesema Aweso.
Spika Tulia alipoangalia video hiyo, aliagiza wizara ya maji ikachimbe visima vya dharura kwa ajili ya kuwasaidia wananchi kupata maji safi na salama, agizo lililopokelewa na Aweso ambaye aliahidi kulifanyia kazi.
“Nimeletewa hapa hizo clip nafikiri msaidizi njoo umfikishie waziri ili apate hii picha. Hali ya wananchi siyo inayokubalika kwenye hivyo visima wanavyochota maji maana yake kwenye hiyo ardhi yako maji ikienda gari kuchimba visima yatapatikana wakati miradi mikubwa ikiendelea wachimbiwe visima,” amesema Spika Tulia.
Leave a comment