MBUNGE Viti Maalum, Dk. Thea Ntara ameitaka Serikali kutoa elimu kwa mabinti juu ya athari za matumizi holela ya dawa za dharura za kuzuia mimba zisizotarajiwa (P2), ili kuwaepusha na matatizo ya kushindwa kupata watoto (utasa). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Mbunge huyo viti maalum kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), ametoa wito huo leo Jumatatu, bungeni jijini Dodoma, baada ya kuihoji Serikali ina mkakati gani wa kuruhusu matumizi ya Sayana Press, kama njia ya uzazi wa mpango badala ya P2 ambayo ina madhara endapo itatumiwa holela.
“Hili suala sasa hivi linatisha, mabinti wanatumia hizo P2 kama unavyotumia panadol yaani hakuna utaratibu, tutafika wakati mabinti hawa hawataweza kupata watoto, je serikali ina mpango gani wa kutoa elimu kwa hao mabinti ili wajue matumizi ya P2 pamoja na hizo ‘Energy drink’,” amesema Dk. Ntara.
Akijibu swali hili, Naibu Waziri wa Afya, Dk. Godwin Mollel ameitaka jamii ishirikiane katika kuhamasisha matumizi salama ya P2 ili kukwepa athari zake hususan kwa mabinti ambao wanatajwa kuongoza kwa matumizi hayo.
“Ni kweli matumizi ovyo ya P2 yanaleta madhara mengi, inasababisha akina mama kupata hedhi ambayo haina mpangilio na wakati mwingine kupata matatizo ya mifupa, sisi wote kwa pamoja tushirikiane kuhamasisha matumizi mazuri ya P2 yanayozingatia ushauri wa kitaalamu,” amesema Dk. Mollel.
Leave a comment