SERIKALI imetakiwa kuweka mkazo katika utekelezaji sheria zinazowaadhibu wanaume wanaotelekeza familia zao hasa watoto waliozaliwa mapacha kuanzia watatu, ili kuhakikisha wanawake hawabebi mzigo wa kuwalea peke yao. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Wito huo umetolewa leo tarehe 12 Januari 2024, bungeni jijini Dodoma na Mbunge wa Ushetu, Emmanuel Cherehani (CCM), aliyesema utekelezaji wa sheria hizo ni mgumu kitendo kinachowafanya wakina mama kuteseka baada ya kukimbiwa na wenza wao wanapojifungua.
“Je, Serikali inatoa kauli gani kwa wanaume wanaozitelekeza familia zao baada ya mke kujifungua watoto mapacha kuanzia watatu,” amesema Cherehani.
Akijibu swali hilo Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mwanaidi Khamis, amesema Serikali imetunga sheria maalum kwa ajili ya kuwapa wazazi wajibu wa kumlea mtoto na kwamba anayekiuka anapewa azabu ya faini isiyozidi Sh. 5,000,000 au kifungo cha miezi isiyozidi sita au vyote kwa pamoja.
Aidha, amewataka wanawake wanaokumbana na kadhia hiyo kutoa taarifa kwa maafisa wa ustawi wa jamii katika maeneo waliyokuwepo ili wapatiwe msaada na serikali kwa kuwa Serikali imeelekeza mamlaka ya serikali za mitaa kupitia halmashauri kuweka bajeti kwa ajili ya kuhudumia watoto wanaotelekezwa na wenye ulemavu.
Leave a comment