WIZARA ya Ofisi ya Rais-Tamisemi, imeiagiza Halmashauri ya Wilaya ya Buhigwe mkoani Kigoma, itumie mapato yake ya ndani, kununua kipimo cha kuchunguza mwili kwa kutumia mawimbi ya sauti (Ultrasound). Anaripoti Jemima Samwel, DMC … (endelea).
Agizo hilo limetolewa leo Jumatatu tarehe 24 Mei 2021, na Naibu Waziri Ofisi ya Rais-Tamisemi, Dk. Festo Dugange, akimjibu Mbunge Viti Maalum (CCM) mkoani Kigoma, Josephine Genzabuke.
Katika swali lake, Genzabuke alihoji lini Serikali itakipatia kituo cha Afya cha Muyama, kilichomo wilayani Buhigwe, vifaa vya Ultrasound na X-Ray.
Akijibu swali hilo, Dk. Dugange amesema kama halmashauri hiyo haina mapato ya kutosha kununua kifaa hicho cha uchunguzi , ikope katika Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF).
“Kituo cha Afya cha Muyana hakitoi huduma ya uchunguzi wa X-Ray na Ultrasound, kutokana na ukosefu wa majengo na vifaa hivyo. Serikali inamuelekeza mganga kununua Ultrasound kupitia mapato ya ndani,” amesema Dk. Dugange.
Kuhusu X-Ray, Dk. Dugange amesema Serikali inajipanga kununua kipimo hicho.
“Ultrasound inunuliwe wakati Serikali Kuu ikitafuta fedha kwa ajili ya kununu X-Ray. Aidha, ikiwa mapato ya ndani ya halmashuri hayatoshelezi, Serikali inamshauri mkurugenzi kukopa fedha kupitia NHIF na kununua mashine ya Ultrasound,” amesema Dk. Dugange.
Leave a comment