MABAO mawili kwenye dakika ya 71 na 76 yalimfanya Sergio Kun Aguero kufikisha mabao 184 ndani ya Ligi Kuu England na kuweka rekodi ya kuwa mchezaji aliyefunga mabao mengi akiwa ndani ya klabu moja. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Kwa idadi hiyo, Aguero amevunja rekodi iliyokuwa ikishikiliwa na Wayne Rooney, ambaye alifunga mabao 183 akiwa na klabu ya Manchester United.
Aguero amepachika mabao hayo kwenye ushindi wa mabao 5-0, ambayo klabu ya Manchester City iliupata kwenye mchezo wa mwisho wa Ligi Kuu England dhidi ya Everton kwenye dimba la Etihad.
Mchezo huo ulikuwa wa mwisho kwa Aguero akiwa amevaa jezi ya Manchester City, baada ya kuripotiwa kuondoka ndani ya klabu hiyo mwishoni mwa msimu huu kuisha kama mchezaji huru.
Mshambuliaji huyo anaondoka ndani ya klabu ya Manchester City, akiwa amecheza jumla ya michezo 374 na kufunga mabao 247 katika michuano yote 10 aliyoitumikia klabu hiyo, toka alipojiunga nayo 2011 akitokea klabu ya Atletico Madrid ya Hispania.
Katika kipindi hicho, Aguero amefanikiwa kutwaa mataji matano ya Ligu Kuu England na kuibuka na tuzo kadhaa kama mchezaji binafsi.
Huenda mshambuliaji huyo akaweka rekodi nyingine siku Jumamosi tarehe 29 Mei, 2021 kwa kutwaa taji la Ligi ya Mabingwa Ulaya katika mchezo wa fainali ambapo klabu yake itashuka Uwanjani dhidi ya Chelsea.
Kuondoka kwa Aguero ndani ya klabu ya Manchester City kumechagizwa na kuandamwa kwa muda mrefu na majeruhi na kukaa nje ya uwanja.
Aguero anaondoka ndani ya Ligi Kuu nchini England huku akiwa na umri wa miaka 32.
Leave a comment