Mbunge wa Ileje ambaye pia ni Naibu Waziri wa Ujenzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya amekabidhi mitungi 107 kwa wajumbe wa halmashauri kuu ya CCM wilayani humo ukiwa ni mwendelezo wa kuhamasisha kampeni ya uhifadhi wa mazingira. Anaripoti Ibrahim Yassin, Songwe…(endelea).
Kasekenya amekabidhi mitungi hiyo kwa wajumbe hao leo tarehe 2 Januari 2024 katika makundi mawili ambapo kundi la kwanza ni wajumbe wa tarafa ya Bundali ambapo zoezi hilo limefanyika katika ofisi za wakala wa misitu Tanzania wilaya ya Ileje (TFS) na kundi la pili limewakutanisha wajumbe wa halmashauri kuu CCM wilayani humo katika ofisi za chama hicho zilizopo Itumba.
Amesema mitungi hiyo itakuwa mwanzo kwa wajumbe wa halmashauri ya wilaya ili wawe chachu ya darasa kwa wananchi wa Ileje kupambama na tatizo la mabadiliko ya tabia nchi.
Ameeleza kuwa matumizi ya gesi hiyo yatasaidia ufanisi kwa akina mama kulinda mazingira na kujiepusha na matumizi ya mkaa.
“Wajumbe hawa watakuwa chachu ya kuleta mabadiliko ya uoto wa asili kutokana na uharibifu wa mazingira kwa ajili ya matumizi ya kuni kwa ajili ya kupikia lakini mitungi hii itaenda kuwa mwarobaini kusaidia mazingira ya Ileje,” amesema.
Amesema ugawaji wa mitungi hiyo 107 ni mwanzo kwani ajenda ya kitaifa ni kupambana na mabadiliko ya tabia nchi ambayo imesababishwa na uharibifu wa mazingira hivyo itakuwa ni mwendelezo kwa makundi mengine.
“Niwahimize wananchi wote wenye kipato kuondokana na matumizi ya kuni na kwenda kwenye matumizi ya gesi kama ilivyo ajenda ya kitaifa ya kukabiliana na manadiliko ya uoto wa asili,” amesema.
Mbunge huyo ambaye amekuwa akipambana kutatua changamoto za jamii, amewashauri wajumbe hao na wadau wengine kumuunga mkono kufanikisha Kampeni ya Pika kwa Gesi, Tunza Mazingira.
Pia amesema kufikia makundi mengine kwenye jamii kwa lengo la kulinda afya za akina mama, kutunza mazingira na kuepusha madhara ya mabadiliko ya tabia nchi, mambo ambayo yatapelekea kuimarisha lishe bora.
Leave a comment