WAKATI Tanganyika ikiadhimisha miaka 62 tangu kupata uhuru, Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, amewataka watanzania kuongeza jitihada za kuleta maendeleo pamoja na kukemea ubaguzi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Mbowe ametoa wito huo leo tarehe 9 Disemba 2023, kupitia kurasa zake za mitandao ya kijamii. Tanganyika huadhimisha siku ya uhuru tarehe 9 Disemba kila mwaka.
“Tunapoadhimisha, naomba tujenge upya mioyo yetu na kuahidi kuwa jasiri tena katika harakati zetu za maendeleo na ustawi. Naomba tuwe hodari katika jitihada zetu za kujenga Tanzania inayojumuisha kila mmoja wetu bila ubaguzi, yenye haki kwa kila mmoja wetu, na yenye neema kwa wote,” ameandika Mbowe.
Mwenyekiti huyo wa Chadema amesema licha ya mafanikio mbalimbali ambayo Tanganyika imepata tangu uhuru, lakini bado inakabiliwa na janga la umasikini kwa watu wake.
“Tunaadhimisha miaka 62 ya uhuru tukikumbuka pia umasikini wa watu wetu katikati ya wingi wa rasilimali, fursa zilizopotea na ahadi zilizovunjwa kutokana na sera na uongozi ambao haukutumia nguvu na ujasiri wa Watanzania,” ameandika Mbowe.
Amewataka Watanzania waenzi juhudi za waliopigania uhuru kwa kulipigania taifa kwa ujasiri pamoja na kukataa ahadi alizoita za uongo.
Leave a comment