RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, amewasamehe wafungwa 2,244, huku akiwabadilishia hukumu wafungwa wawili kutoka adhabu ya kifo na kuwa kifungo cha maisha jela. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Taarifa ya msamaha huo imetolewa leo tarehe 9 Disemba 2023 na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni, ikiwa Tanzania Bara inaadhimisha miaka 62 ya uhuru.
Miongoni mwa wafungwa waliopatiwa msamaha huo ni wale wenye magonjwa sugu ambao wapo katika hatua ya mwisho iliyothibitishwa na mganga mkuu wa mkoa au wilaya. Wafungwa wa maisha ambao wametumikia vifungo vyao kwa muda wa miaka 15 na kuendelea.
“Wafungwa 2,244 wamenufaika na msamaha huu ambapo 263 wataachiliwa huru leo. Wafungwa 2 waliohukumiwa adhabu ya kifo wamebadilishiwa adhabu na kuwa kifungo cha maisha na wafungwa 1,979 wamepunguziwa sehemu ya adhabu zao ambazo wataendelea kuzitumikia gerezani,” imeandika taarifa ya Mhandisi Masauni na kuongeza:
“Ni matumaini ya Serikali kwamba wafungwa walioachiliwa huru leo watarejea tena katika jamii kushirikiana na wananchi wenzao katika ujenzi wa taifa letu na kwamba watajiepusha kutenda makosa ili wasirejee tena gerezani.”
Leave a comment