RAIS wa Marekani, Joe Biden ametangaza kuwa nchi hiyo yake imepiga marufuku ununuzi wa gesi, mafuta na makaa ya mawe kutoka Urusi. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Jana tarehe 8 Machi, 2022 Rais Biden ametangaza marufuku hiyo ya kuagiza bidhaa za mafuta na nishati kutoka Urusi kama njia mojawapo ya kuiadhibu nchi hiyo iliyoamua kuivamia kivita taifa la Ukraine.
“Tunapiga marufuku uagizaji wa bidhaa zote za mafuta na gesi kutoka Urusi. Hatua hiyo inamaanisha kuwa bidhaa zote za nishati hazitakubaliwa kusafirishwa katika bandari ya Marekani,” Rais Biden aliwaambia waandishi wa habari Ikulu ya White House.
Wakati hayo yakijiri taifa la Uingereza limesema kwamba litapiga marufuku ununuzi wa mafuta hayo pamoja na bidhaa nyinginezo za nishati mwishoni mwa mwaka huu.
Aidha, limewaruhusu wafanyabiashara na wasambazaji wa bidhaa hiyo kwa muda huku wakiendelea kutafuta njia mbadala.
Naye Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani, Annalena Baerbock amenukuliwa na Shirika la habari la Ufaransa (AFP) akisema kuwa, nchi yake inapinga vikwazo vya kutoagiza bidhaa za nishati kutoka Urusi.
Baerbock amesema iwapo Ujerumani itazuia kuingiza nchini humo kwa bidhaa hizo kutoka Urusi, umeme utakatika nchini humo hivyo watalazimika kuviondoa vikwazo hivyo wao wenyewe ili uchumi wake usisambaratike.
Taifa la Ujerumani linategemea kwa asilimia 55 gesi na asilimia 42 ya mafuta na makaa ya mawe vyote kutoka Urusi.
Leave a comment