Wizara ya mambo ya nje ya Marekani imeziagiza familia za wanadiplomasia na wafanyakazi wasio wa dharura kwenye ubalozi wa Marekani mjini Kiev kuondoka Ukraine. Anaripoti Theresia Mpambije… (endelea)
Pia imewahimiza raia wote wa Marekani walioko Ukraine kufikiria kuondoka nchini humo, kutokana na tishio linaloendelea kuongezeka la uvamizi kutoka Urusi.
Katika tahadhari ya usafiri iliyochapishwa kwenye tovuti yake, wizara ya mambo ya nje imesema kulikuwa na taarifa kwamba Urusi inapanga hatua kubwa za kijeshi dhidi ya Ukraine.
Tangazo hilo limekuja huku kukiwa na wasiwasi miongoni mwa mataifa ya magharibi na Ukraine juu ya ongezeko la wanajeshi wa Urusi kwenye mpaka wake na Ukraine.
Tarehe 22 Januari mwaka huu, wizara ya mambo ya nje ya Uingereza ilidai kuwa Urusi inataka kumuweka kiongozi anaegemea upande wake nchini Ukraine, madai ambayo Urusi iliyataja kuwa upotoshaji.
Waziri wa ulinzi wa Ujerumani, Christine Lambrecht ametoa wito wa kutuliza mzozo katika mahojiano siku ya Jumamosi, na kuongeza kuwa Ujerumani haitoipatia silaha Ukraine.
Mkuu wa muungano wa ulinzi wa kijeshi wa NATO, ameonya kwamba kuna hatari ya mzozo mpya wa Bara la Ulaya baada ya vikosi vya Urusi vinavyokadiriwa kuwa 100,000 kukusanyika mpakani.
Jumamosi, tani zipatazo 90 za ‘misaada hatari’ ya Marekani zikiwemo risasi kwa ajili walinzi walio mstari wa mbele ziliwasili Ukraine.
Waziri wa Mambo yanje wa Marekani, Anthony Blinken alisema serikali inachukua hatua stahiki ambazo zitabaini mahesabu ya Rais wa Urusi, Vladimir Putin ikiwa ni pamoja na kuongeza ulinzi Ukraine kwa usaidizi zaidi wa kijeshi.
Urusi iliwahi kuchukua eneo la Ukraine ambalo liliitenga na Ukraine katika mwaka 2014, baada ya nchi hiyo kumpindua rais aliyeungwa mkono na Urusi.
Tangu wakati huo, jeshi la Ukraine limekuwa katika vita na waasi wanaoungwa mkono na Urusi katika maeneo ya mashariki mwa nchi hiyo karibu na mipaka yake na Urusi. Inakadiriwa kuwa watu 14,000 waliuawa katika jimbo ka Donbas kufuatia mzozo huo.
Leave a comment